Thursday, April 23, 2015

SHINDANO LA TMT 2015 LAZINDULIWA RASMI LEO, MWANZA KUFUNGUA PAZIA TAREHE 24 APRIL 2015.

Afisa Masoko na Mahusiano wa Proin Promotions Ltd, Josephat Lukaza akizungumzia Uzinduzi wa msimu wa pili wa Shindano la TMT 2015 lililopo chini ya Kampuni ya Proin Promotions Ltd ambao pia ni wasambazaji, wauzaji na watengenezaji wa filamu za Kitanzania. Anayeshuhudia pembeni ni Mratibu wa Masoko wa ITV/Radio One ambao ni mmoja wa wadhamini wa Shindano la TMT 2015.
 Mratibu wa masoko kutoka ITV/Radio One (wa pili kulia) akizungumzia juu ya umuhimu wa wao ITV/Radio one kuwa washirika wa TMT 2015 na kuhaidi makubwa zaidi kwa mwaka 2015.P
 Mmoja wa majaji wa shindano la TMT 2015 Yvonne Cherry au Monalisa akizungumza mbele ya waandishi wa habari(hawapo pichani) kuhusiana na shindano la TMT 2015 lililozinduliwa rasmi leo jijini Dar Es Salaam
…………………………………………………………………..

Shindano la Tanzania Movie Talents (TMT) 2015 limezinduliwa rasmi leo huku baadhi ya vigezo vikiwa vimeboreshwa, akizungumzia hayo Meneja wa Mradi wa TMT 2015, Saul Mpock amesema kuwa “Mwaka Huu Kigezo kimojawapo ni mshiriki kuwa na umri kuanzia miaka 16 na kuendelea huku fomu za kushiriki shindano hilo zikipatika siku ya usaili katika mkoa husika na bila gharama yoyote”

Shindano la Tanzania Movie Talents 2015 linaanza rasmi Kesho huku Kanda ya Ziwa ndio itakayofungua pazia la shindano hili kwa Mwaka 2015, Shindano hili linafanyika kikanda ambapo kanda sita za Tanzania zitafikiwa na shindano hili.

Kwa kanda ya Ziwa usaili utaanza tarehe 24 Aprili 2015 huku zoezi zima likifanyika mkoani Mwanza na hatimaye zoezi kuendelea kanda ya Kaskazini, Arusha, Kanda ya Kati, Dodoma, Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Mbeya, Kanda ya Kusini, Mtwara na Kumalizika Kanda ya Pwani, Dar Es Salaam.

Katika kanda zote tano ikiwa Kanda ya Ziwa, Kaskazini, Kati, nyanda za juu kusini na Kusini Washindi watakuwa ni watatu kutoka kila kanda ambapo kila mshindi ataibuka na kitita cha shilingi laki tano kila mmoja huku kanda ya Pwani itatoa washindi watano na kila mmoja kuondoka na shilingi laki tano pia na kupelekea Washindi kuwa 20 na kuingia kwenye nyumba ya TMT kwaajili ya Hatua ya Mchujo.

TMT 2015 itarushwa na kituo cha ITV siku ya Jumapili saa tatu usiku huku kipindi cha kwanza kabisa cha TMT kikitarajiwa kuonekana tarehe 10 May 2015.

Shindano hili la TMT 2015 limedhaminiwa na Kampuni ya Usafirishaji ya Precision AirI-View StudioGlobal Publishers na Kituo cha ITV/Radio One ambao ndio watakaokuwa wakirusha matangazo ya TMT 2015. TMT ikiendelea kupata sapoti kutoka katika vituo mbalimbali za redio mikoani. Vilevile tunatoa nafasi kwa makampuni mengine ambao wangependa kushirikiana na TMT kwa mwaka 2015

Kauli Mbiu ya TMT 2015 ni Mpaka Kieleweke.

No comments: