Thursday, January 10, 2013

Wanafunzi walioongoza mtihani wa taifa wa darasa la saba wa mwaka 2012

 Wanafunzi walioongoza mtihani wa taifa wa darasa la saba wa mwaka 2012, Janeth Kijazi (kushoto) Justina Kalala (katikati)na Kellen Mudogo wakiwa shule ya sekondari ya wasichana, St Marian Bagamoyo, jana, walikoanza kidato cha kwanza. Wanafunzi hao walihitimu elimu ya msingi katika Shule ya Tusiime ya jijini Dar es Salaam. Picha Florence Majani wa MWANANCHI  
&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&&
 
Florence Majani
WANAFUNZI walioongoza mtihani wa Darasa la Saba kitaifa mwaka jana, ni wasichana watatu waliokuwa wanasoma katika Shule ya Msingi Tusiime iliyoko Dar es Salaam, imefahamika.
Wasichana hao, Justina Kalala, Janeth Kijazi na Kellen Mudogo waliongoza mtihani huo wenye masomo matano kwa kila mmoja kupata alama 234 kati ya 250.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, mabinti hao ambao wote wanasoma kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Marian, Bagamoyo, walisema siri ya mafanikio yao ni maombi na nia ya kutaka kufaulu.

Justina alisema siri ya kufaulu mitihani yake ni kumtanguliza Mungu kabla hajafanya kitu chochote hata kama ni majaribio ya kawaida darasani... “Pia elimu bora ninayopewa na wazazi wangu nayo inanipa nguvu ya kusoma kwa bidii.”

Justina alisema siri nyingine ya kufaulu kwake katika mitihani hiyo ni kusoma na kisha kuwafundisha wenzake kile alichokielewa. Alisema jambo hilo lilimjengea uwezo wa kuyashika yale aliyoyasoma.

“Nilikuwa nawakusanya wenzangu katika makundi ili tusome.”
Mwanafunzi huyo ambaye alipokuwa shule ya msingi aliteuliwa kuwa mratibu wa taaluma kutokana na kuwaongoza wenzake katika vikundi vya kujisomea, alisema anatamani kuwa mfamasia pindi atakapofanikiwa kumaliza masomo yake na kufaulu.

Pia, Janeth ambaye alisema ufaulu wake ulimtegemea zaidi Mungu, anapenda zaidi masomo ya sayansi... “Nataka kuwa daktari ndiyo maana najitahidi zaidi katika masomo ya sayansi. Nilipokuwa shule ya msingi nilikuwa naweka juhudi zaidi katika somo la hesabu na baiolojia.”

Alisema alipokuwa msingi, alikuwa ni kiongozi wa kikundi cha kujisomea na alikuwa anatumia muda wake mwingi kusoma vitabu na kuwauliza walimu kile ambacho alikuwa hakijui.

Kwa upande wake, Kellen mbali na kusema kwamba anamtegemea Mungu zaidi katika masomo yake, alitoa siri nyingine ya kushinda katika mtihani huo kuwa ni kurudia kile walichofundishwa na kutumia vyema muda wake.

Kellen alisema anapenda masomo ya sayansi na anatamani kuwa daktari endapo atafaulu masomo yake ya Chuo Kikuu.

Walikuwa na msukumo
Aliyekuwa mwalimu wa darasa wa wanafunzi hao huko Tusiime, Valentine John alisema wanafunzi hao walikuwa na msukumo wa ndani wa kusoma tofauti na wengine.
“Pia wameandaliwa vyema tangu chekechea ndiyo maana wamefanya vizuri, sisi haitushangazi wao kuongoza kwa sababu tuliujua ubora wao tangu zamani,” alisema.

Mwalimu huyo alisema wanafunzi hao watatu walikuwa si wakorofi, bali wasumbufu kwa walimu katika mambo wasiyoyajua.

No comments: