Tuesday, January 08, 2013

TAARIFA KWA WANANCHI KUHUSU KUFUNGWA KWA MAUZO YA NYUMBA ZA MAKAZI ZA KIGAMBONI HOUSING ESTATE ZILIZOKO KIGAMBONI DAR ES SALAAM


Shirika la Nyumba la Taifa lililizindua mchakato wa mauzo ya nyumba za Makazi za Kigamboni (Kigamboni Housing Estate) tarehe 20 Desemba 2012, ili kuwapatia Watanzania walioko ndani na nje ya nchi kupata muda wa kujiandaa kwa ajili ya tarehe rasmi iliyoandaliwa kwa ajili ya kuanza kupokea rasmi pesa. Fursa hiyo ililenga kuwapa nafasi pia watu walioko nje ya nchi, waliosafiri kipindi cha sikukuu na vile vile ilizingatia maoni ya wateja wetu ambao wamekuwa wakipendekeza kupata taarifa ya kuanza mauzo kuanzia wiki moja na zaidi ili waweze kijipanga.

Kuanzia tarehe 2 Januari 2013, maombi yalianza kupokelewa na mwitikio umekuwa mkubwa sana. Tumepokea maombi zaidi ya asilimia 120 ya idadi ya nyumba 182 zinazouzwa. Tunawapongeza sana wananchi kwa kuitikia wito wa kununua nyumba za makazi za Kigamboni Housing Estate.
 Kama utaratibu wa mauzo unavyotaka, tukishapokea maombi zaidi ya asilimia 120 lazima tutangaze kufungwa kwa mauzo ya nyumba husika. Mnamo tarehe 3 Januari 2013 tulifunga rasmi mauzo ya nyumba hizo baada ya kufikia lengo hilo kwa mradi huu wa Kigamboni kwa sasa.

Tunapenda kusisitiza kuwa tumefunga zoezi la kupokea pesa kutoka kwa wanunuzi wa nyumba za mradi huu wa Kigamboni. Hata hivyo, kumalizika kwa mauzo ya nyumba hizi za Kigamboni, ni mwanzo wa kuanza mauzo ya nyumba za miradi mingine mingi ya nyumba za gharama nafuu ambayo zinazondelea kujengwa na Shirika hapa Dar Es Salaam na maeneo mengine  nchini. Miradi mingine ya nyumba za gharama nafuu  inayotekelezwa kwa sasa sambamba na mradi huu wa Kigamboni ni pamoja na Mwongozo Housing Estates (Dar Es Salaam) na miradi mingine inayoendelea katika Mikoa 14 nchini.

Mikoa na Wilaya zenye miradi ya nyumba za gharama nafuu kwa sasa ni pamoja na Mvomero (Morogoro), Kongwa (Dodoma), Ilembo (Katavi), Geita, Mkinga (Tanga), Babati (Manyara), Monduli na Longido (Arusha), Mkuzo (Songea) na Unyankumi (Singida).

Hivyo, tunawashauri wananchi waendelee kujiandaa zaidi kwa kuweka akiba ya fedha na vile vile kuendelea kufanya mawasiliano na benki ambazo zinaushirikiano na Shirika la Nyumba la Taifa ili waweze kufanyiwa tathmini ya mikopo yao ya nyumba, ili mara tu taarifa za mauzo ya nyumba katika Miradi zitakapotoka waweze kununua nyumba hizo. Benki ambazo tunashirikiana nazo ni pamoja na Commercial Bank of Africa (CBA), NBC, NMB, AZANIA BANK, BANK OF AFRICA(BOA) na Banc ABC. Benki zingine ni EXIM BANK, KCB na Stanbic Bank.

Tunawashukuru sana wateja wetu kwa kutuunga mkono ili kulijenga Taifa letu..

Pamoja Tunaweza

   Imetolewa na;

Kitengo cha Mawasiliano ya Umma na Huduma kwa Jamii.
Shirika la Nyumba la Taifa.

No comments: