Wednesday, January 09, 2013

MWANDISHI WA HABARI ISSA NGUMBA AMEUAWA KIGOMA


MWANDISHI wa Habari wa kituo cha Radio Kwizera wilayani Kakonko mkoani Kigoma, Issa Ngumba (45) (Pichani juu) ameua kwa kunyongwa na kisha kupigwa risasi mkono wa kushoto huku simu zake mbili na Bastora iliyotumika kumshambulia ikiacha kando ya mwili wake porini.
Habari ambazo zimepatikana na kutoka wilayani Kakonko mkoani Kigoma na kuthibitishwa na kamanda wa Polisi mkoa wa Kigoma Frasser Kashai, pamoja na Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa Habari Kigoma (KPC) Deo Sonkolo imedai mwandishi huyo amekutwa ameuawa kwa kunyongwa shingo na watu ambao hawajajulikana.
Akizungumza na gazeti hili jana kwa njia ya simu, Sonkolo alisema kwamba mara baada ya kupata taarifa waliwasiliana na waandishi wa wilaya ya Kibondo ambao waliwahi kufika eneo la tukio na kushuhudia uchunguzi wa Daktari Primus Ijumaa aliyeeleza kuwa mwili wa marehemu umenyonga ikiwa ni pamoja na kupigwa risasi mkono wa kushoto.
Mwili wake umepatikana jana katika pori la Mlima Kajuluheta kijiji cha Muhange, wilayani humo majira ya asubuhi baada ya wananchi kufanya msako wa siku tatu tokea Jumapili siku moja baada ya kutoonekana kwake.
“Sisi tunaelekea wilaya ya Kakonko toka Kigoma mjini, lakini walioshuhudia mwili huo huko eneo la tukio waneleza kwamba kando ya mwili wake kumekutwa Bastora moja, haijafahamika iwapo ilikuwa inamilikiwa na marehemu ama nani, simu zake mbili na kwa mujibu wa Dkatari maiti inaonekana kunyongwa shingo na kupigwa risasi mkononi,” alieleza Sonkolo.
Imeelezwa kwamba bastora iliyokutwa eneo la tukio imekutwa na ikiwa na risasi tano huku mifuko ya suruali ya marehemu ikiwa na noti moja ya Tsh10,000.
Kwa upande wake kamanda wa Polisi mkoa wa Kigoma Frasser Kashai akithibitisha kuwapo kwa tukio hilo lakini alisema kwa sasa jeshi lake linangoja taarifa ya daktari aliyefanya uchunguzi wa mwili wake ikiwa ni pamoja na taarifa ya awali ya uchunguzi wa jeshi hilo toka eneo la tukio.
Aidha akizungumza na gazeti hili Naibu Mharari wa kituo cha Radio Kwizera kinachorusha matangazo kutoka wilayani Ngara mkoani Kagera, Seifu Upupu, alisema kwamba tokea Januari 5 mwaka huu walikuwa majira ya saa 11 walikuwa wakijaribu kuwasiliana naye na simu zake zilikuwa zikiita bila ya kupokelewa mpaka jana ambapo zilikuwa hazipatikani.
“Maelezo kutoka kwa mke wake Rukia Yunus ni kwamba Marehemu aliondoka nyumbani kwake jioni na kumuaga mkewe kuwa alikuwa akienda madukani (center) lakini tokea hapo hakurudi wala kuonekana ambapo ilipofika Jumapili serikali ya kijiji ilianzisha msako mkali kumsaka mpaka jana asubuhi walipokutana na mwili wake porini,” alieleza Mhariri huyo.
SOURCE:MWANANCHI

No comments: