Monday, February 15, 2010

watano wafa kwa kuangukiwa na kifusi

Watano wafariki dunia
kwa kufukiwa na kifusi

Israel Mgussi, Dodoma

WATU watano wamefariki dunia papo hapo na wengine wawili kujeruhiwa baada ya kufunikwa na kifusi kwenye machimbo ya kokoto yaliyopo katika kijiji cha Ntyuka, nje kidogo ya mji wa Dodoma.

Kwa mujibu wa Kaimu Kamanda wa Polisi mkoa wa Dodoma, Salum Msangi, waliopoteza maisha katika tukio hilo kuwa ni Mwajuma Mnubi, Monika Chizumi, Mbeleje Ndigomba wote wakazi wa kijijini hapo na Jonasi Mnubi (2) na jina la marehemu mmoja halikupatikana. Hata hivyo, majina ya waliojeruhiwa hayakuweza kupatikana.

Msangi alisema tukio hilo lilitokea mnamo saa 5 asubuhi, lakini polisi walipata taarifa majira ya saa 6 mchana na kwamba, uokoaji ulianza saa 7 mchana hadi saa 10 jioni.

“Tulifika eneo la tukio kwenye saa 7 mchana na kuanza kufukua kifusi tukisaidiana na wafanyakazi wa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA)ambao walitoa katapila lililosaidia kwa kiasi kikubwa kufukua udongo,” alisema.

Mashuhuda hao walisema, marehemu hao ambao walisimama kwenye gema karibu na shimo hilo, walijikuta katika wakati mgumu baada ya udongo wa mahali walipokuwa wamesimama kumeguka na kutumbukia shimoni na kufukiwa kabisa.

Kutokana na shimo hilo kuwa kubwa walishindwa kutoka na wala watu wengine walishindwa kuwanusuru kutokana na kiasi kikubwa cha udongo uliowafunika.

“Tukio hili lilitokea muda wa saa tano asubuhi, lakini tulishindwa kuwaokoa wakiwa hai kutokana na kiasi kikubwa cha udongo kilichomeguka na kufunika kabisa shimo, hivyo tuliamua kuomba msaada polisi na uokoaji ulianza rasmi saa saba mchana baada ya wanausalama hao kufika,” walisema mashuhuda wa tukio hilo.

Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Dk James Msekela alishiriki kikamilifu katika ufukuaji wa shimo hilo na alitoa kiasi Sh50,000 kwa kila familia ya marehemu hao na kuwatahadharisha watu wanaojihushisha na uchumbaji wa kokoto kuwa makini ili wasije wakakumbwa na balaa kama hilo.

Kijiji cha Ntyuka ni maarufu kwa shuguli za uchimbaji wa kokoto zinazotumika katika ujenzi na asilimia 80 ya shughuli za ujenzi mjini Dodoma hutegemea kokoto za kutoka eneo hilo.

No comments: