Tuesday, February 16, 2010

Msekwa ammwagia sifa Spika Sitta


Makamu Mwenyekiti wa CCM (Tanzania Bara) Pius Msekwa akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari mjini Dodoma leo. Kulia ni Katibu wa Itikadi na Uenezi wa NEC, John Chiligati. Picha na Jube Tranquilino.

*************************************************

MAKAMU Mwenyekiti wa CCM, Pius Msekwa amemmwagia sifa Spika wa Bunge Samuel Sitta kwa kile alichoeleza kuwa amefanikiwa kumaliza sakata la Richmond kwa busara kubwa.
 
Akizungunza na waandishi wa habari jana mjini Dodoma leo, Msekwa alisema sababu ya uhasama wa wabunge wa CCM, Msekwa alisema yalitokana na sakata lililoibuliwa mwanzoni mwa mwaka 2007 na kusababisha mtikisiko mkubwa ndani ya serikali ya awamu ya nne.

CCM iliingia kwenye mtafaruku uliotengeneza makundi mawili makubwa mwaka 2008 baada ya sakata la Richmond kutinga bungeni na kisha kuwakumba baadhi ya makada wa juu wa chama hicho, waliotuhumiwa kuhusika na kashfa hiyo ya kifisadi iliyotokana na zabuni tata ya uzalishaji umeme wa dharura iliyoipa ushindi kampuni hiyo(Richmond).

Baadhi ya makada wa chama ngazi za juu katika chama na serikali, akiwemo aliyekuwa Waziri Mkuu, Edward Lowassa na mawaziri wawili walioitumikia Wizara ya Nishati na Madini kwa nyakati tofauti wakati wa mchakato wa zabuni hiyo, Dk Ibrahim Msabaha na Nazir Karamagi walilazimika kujizulu kutokana na kudaiwa kuhusika katika sakata hilo, huku maofisa wengine wa umma wakitakiwa kuchukuliwa hatua na serikali.
 
Alisema baada ya sakata hilo kulipuka kulitokea mgawanyiko mkubwa katika chama uliozaa makundi mawili. Alitaja vinara wa makundi hayo kuwa ni mbunge wa Monduli Edward Lowassa na Spika wa Bunge, Samuel Sitta.
 
Kwa mujibu wa Msekwa makundi hayo kila moja lilikuwa likituhumu kundi jingine kuwa lina nia ya kuwang’oa wenzao madarakani, jambo hilo lilileta mtafaruku mkubwa.
 
“Tumewaita vinara wa makundi hayo na kukaa nao meza moja. Lakini hatukuwa na nia ya kutaka kuwatoa kafara kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari, bali tulitaka amani idumu jambo linaloonyesha kuwa tumefaulu,” alisema Msekwa na kuongeza:
 
“Pamoja na kukaa nao kwa muda wa saa nne katika moja ya kumbi za pale bungeni, kila mmoja alikuwa na kero zake jambo tulilogundua kuwa kila mtu alikuwa akifagilia kitumbua chake kisiingie mchanga”.
 
Katika kile kinachoweza kutafsiriwa kama ni kumtonesha kidonda jana Mbunge wa Igunga, Rostam Aziz, Msekwa alimfagilia spika Sitta kwa kumaliza sakata la Richmond na kisha kuonya kuwa watakaoliendeleza watachukuliwa hatua.
 

No comments: