Thursday, February 11, 2010

Babu Seya, Papii basi tena!!!

Babu Seya akisindikizwa Jela

Shangazi ya Babu Seya akilia kwa uchungu

WANAYE WAWILI WAACHIWA, YEYE NA PAPII NGUZA WAKWAMA

HUKUMU ya Mahakama ya Rufaa, iliyotolewa na jopo la majaji watatu leo hii imeibua vilio na majonzi baada ya kumtia hatiani mwanamuziki maarufu nchini mwenye asili ya Kongo, Nguza Viking maarufu kama Babu Seya na mwanaye Johnson Nguza hivyo kuendelea kutumikia kifungo cha maisha jela.

Hata hivyo, mahakama hiyo iliwaacha huru wanaye wengine wawili, Nguza Mbangu na Francis Nguza baada ya kubainika kuwa hawana hatia.

Babu Seya na wanaye, Johnson Nguza maarufu kama Papii Kocha, Nguza Mbangu na Francis Nguza walihukumiwa kifungo cha maisha mwaka 2004, baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwatia hatiani kwa makosa ya kubaka na kuwalawiti watoto wa kike waliokuwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Mashujaa jijini Dar es Salaam.

Hata hivyo walikata rufaa Mahakama Kuu ambako Jaji Thomas Mihayo (mstaafu kwa sasa), aliwatia hatiani na kuunga mkono hukumu ya Hakimu Mkazi Mkuu, Addy Lyamuya; kisha wakakata rufaa katika Mahakama ya Rufaa.

Katika hukumu ya Mahakama ya Rufaa, iliyotolewa na jopo la majaji watatu, Salum Massati , Mbarouk Mbarouk, wakiongozwa na Jaji Nathalia Kimaro waliosikiliza rufaa hiyo, iliyosomwa jana na Naibu Msajili wa Mahakama ya Rufaa (DRCA), Neema Chusi, Babu Seya na mwanaye Papii Kocha walitiwa hatiani, huku Nguza Mbangu na Francis Nguza wakiachiwa huru.

Wakati akitoka nje ya mahakama kuelekea gerezani, Babu Seya aliendelea kusisitiza kuwa hakufanya kosa hilo na asingeweza kufanya hivyo na watoto wake, huku mwanaye Papii Kocha akisema kuwa wanategemea huruma ya Rais Kikwete na kwamba, wana imani kuwa atawatoa.

Wakili wao Mabere Marando alisema, "Tumeshinda nusu, tumeshindwa nusu. Huo ni uamuzi wa mahakama na kuwa hajawa na mpango wa kuendelea zaidi ya hapo."

Akisoma hukumu hiyo, Chusi alisema mahakama imeridhika na ushahidi ulioko kwenye kumbukumbu za mwenendo wa kesi hiyo kwa kila kosa na kwamba mrufani wa kwanza (Babu Seya) na wa pili (Papii Kocha), walihusika katika kutenda makosa na kwamba, utetezi wao kuwa hawakuwepo katike eneo la tukio ulikataliwa.


Kwa mujibu wa hukumu ya Mahakama ya Rufaa, Babu Seya alitiwa hatiani kwa makosa matano ya kubaka na Papii Kocha alitiwa hatiani kwa makosa mawili, wakati Mbangu na Francis hawakupatikana na hatia kwa makosa yote.

“Mrufani wa kwanza amepatikana na hatia ya makosa mawili ya ubakaji kosa la 7 na la 12 kinyume cha kifungu cha 130 (2)(e) na 131A vya Kanuni ya Adhabu (Penal Code) kama vilivyorekebishwa na vifungu vya 5 na 7 vya SOSPA (Sheria ya Makosa ya Kujamiiana),” ilisema hukumu hiyo na kuongeza:

Kwa kosa la 10 na 18 warufani namba moja (Babu Seya) na namba 2 (Papii Kocha) wamepatikana na hatia ya ubakaji kinyume cha kifungu cha 131A cha Kanuni ya Adhabu.

Hata hivyo katika kosa la 1,3,5,14, 20 na 22, warufani wote hawakupatikana na hatia, wakati katika kosa la 7 na 12 mrufani namba 1 mpaka namba 4 hawakupatikana na hatia huku kosa la 10 na 18 yakiwaondoa mrufani wa tatu (Mbangu) na wa nne (Francis).

“Hatimaye, hatia kwa mrufani namba tatu na wa nne inatanguliwa na hukumu pamoja na amri ya fidia inatupiliwa mbali. Wamewekwa huru isipokuwa kwa sababu nyingineyo. Na kwa mrufani wa kwanza na wa pili amri ya fidia bado inasimama tu kwa makosa ambayo yamewatia hatiani na inatupiliwa mbali kwa makosa yaliyobaki ambayo hayakuwatia hatiani,” ilisisitiza hukumu hiyo.

Mara baada ya Chusi kusoma hukumu hiyo majira ya saa 4:22 asubuhi, baadhi ya warufani hao waliangua kilio wakiwa kizimbani hususan Francis ambaye aliangua kilio kwa sauti kuu, huku Papii Kocha machozi yakimtiririka, lakini Babu Seya na Mbangu wakionekana kujawa na huzuni.

Chusi alianza kusoma hukumu hiyo kwa kuelezea kumbukumbu za mwenendo mzima wa kesi hiyo, akielezea ushahidi uliotolewa na mashahidi wa pande zote katika kesi ya msingi, hukumu ya rufaa ya kwanza ya Mahakama Kuu na hoja zilizotolewa na pande zote katika rufaa zote.

Kisha alisema; “Suala lililoko mbele yetu sasa ni kama ushahidi katika kumbukumbu ulithibitisha utendaji wa kosa. Kama ambavyo tayari imeshaonyeshwa PW 9 (Shahidi wa tisa wa upande wa mashtaka alikuwa ni mtoto wa miaka saba na alitoa ushahidi bila kiapo, ushahidi wake ulihitaji kuungwa mkono."

Katika ushahidi kwenye kumbukumbu hakuna mashaka kuwa PW9 alibakwa. Alithibitisha na kulikuwa na ushahidi wa PW20 kuwa PW9 alibakwa na PW9 alisema waomba rufaa ndio walimbaka.

Alisema jambo la msingi lilikuwa ni kuthibitsha kama waomba rufaa ndio walimbaka.

“Tumekwishatoa maoni juu ya mashahidi wa upande wa mashtaka na hatuhitaji kurudia kile ambacho tumekwishakisema. Inatosha kusema kwamba, kwenye kumbukumbu kuna ushahidi wa kutosha kuonyesha kuwa watoto walikuwa na uwezo wa kuingia katika nyumba ile bila kuonekana,” alisema Chusi.

Alisema kwa mujibu wa uchunguzi wa hali ya nyumba iliyodaiwa kufanyika makosa yale kupitia kwa PW13, unaonyesha kuwa kulikuwa na mlango ambao ungeweza kutumiwa na watoto kuingia ndani ya nyumba ile namba 607 bila kuonekana.

Alisema kilichounga mkono ushahidi huo ni mazingira ya chumba cha mrufani wa kwanza (Babu Seya) ambamo ndimo kulimodaiwa kufanyiwa ubakaji, ambapo PW9 alieleza kuwa kuna godoro kitandani na godoro lingine ukutani na kwamba watoto wengine walikuwa wakilazwa kitandani na wengine kwenye godoro sakafuni.

“Tumesema mwanzoni mwa hukumu hii kuwa waathirika wa makosa ya ubakaji walikuwa ni watoto 10 na ushahidi wao katika maelezo yao kuhusu chumba cha mrufani wa kwanza unafanana,” alisema.

Akizungumzia utetezi wa Babu Seya kuwa alikuwa na matatizo ya nguvu za kiume na hivyo asingeweza kutenda kosa kama hilo na kwamba upande wa mashtaka ulikataa kwenda kumpima ili kuthibitishwa na daktari kama ana uwezo au hana uwezo wa kutenda kosa la ubakaji, mahakama iliutupilia mbali.

“Kwa maoni yetu upande wa mashtaka haukuwa na wajibu wa kufanya hivyo,” alisema Chusi katika hukumu hiyo na kuongeza:

“Tunasema hivyo kwa sababu katika kifungu cha 114 (1) cha Sheria ya Ushahidi (LEA) sura ya 6 kama ilivyorekebishwa mwaka 2002 suala la uwezo wa nguvu za kiume za mrufani ilikuwa katika ufahamu wake na suala la kuthibitisha lilikuwa juu yake kuthibitisha kuwa uume wake haukuwa ukifanya kazi”.

Mahakama pia iliongeza kuwa ingawa kulikuwa na mazoezi katika nyumba hiyo(wanamuziki wa Bendi ya Akudo) haikuwa sababu ya kumzuia mrufani wa kwanza kutenda makosa kwa kuwa, kwa mujibu wa ushahidi matukio hayo yalikuwa yakifanyika kwa muda mfupi sana wakati wa mapumziko na wakati watoto hao wakitoka shule.

“Zaidi hakuna sababu kwa nini watoto wote hao waseme uongo dhidi yake na alikiri kuwa hakuwa na uhasama na mmoja wapo,” iliongeza.

Kuhusu mrufani wa pili Papii Kocha, mahakama katika hukumu hiyo ilisema utetezi wake kuwa hakuwepo hauondoi uwezekano wa kutenda kosa.

“Tunasema hivyo kwa sababu kama ambavyo tumekwishaonyesha makosa yalikuwa yakitendeka kwa muda mfupi kama saa moja tu. Hii ina maana kwamba, hata kama mrufani wa pili alikuwa akifanya shughuli za kutumbuiza nje ya Dar es Salaam, lakini kuna wakati ambao alikuwa Dar es Salaam;

Kwa mujibu wa utetezi wake alikuwa akitoka nje ya Dar es Salaam kwa vipindi na si muda wote. Kwa namna hiyo hatuoni sababu yoyote PW8 ( mmoja wa watoto waathirika) kutengeneza ushahidi dhidi yake. Alikuwa ni mtoto mdogo ambaye hakujua hatari iliyokuwa mbele yake kwa kujihusisha katika, matendo ya ngono katika maisha yake”.

Katika hukumu hiyo mahakama ilichambua ushahidi wa kila mtoto na kueleza jinsi ulivyoweza kuungwa mkono na mashahidi wengine, wakiwemo madaktari waliowafanyia vipimo baadhi ya watoto hao na kuthibitisha kuwa walikuwa wameingiliwa.
SOURCE: MWANANCHI Imeandikwa na James MAGAI na HUSSEIN Kauli

No comments: