Monday, February 08, 2010

Zantel yavuna wateja milioni 1.4


BAADA ya kununua vifaa vya kisasa pamoja na kutumia teknolojia ya kisasa kwa gharama nafuu kupitia uhusiano wake na Etisalat yenye wateja zaidi ya milioni 95 barani Afrika, mashariki ya kati na bara la Asia kampuni ya simu ya Zantel imeongeza idadi ya wateja wake hadi kufikia 1.4 milioni.

Kwa mujibu wa Mkuu mpya wa kitendo cha Biashara Zantel, Norman Moyo alisema kuwa Kampuni hiyo ndani ya hiyo miezi 18 imewekeza zaidi ya dola za kimarekani milioni 140 katika kuboresha mtandao wake na mafanikio yaliyopatikana ni ishara ya uwekezaji huo.

"Uwekezaji huu umejihidhirisha kwenye huduma kwa wateja wa Zantel na wateja wetu wameongezeka kutoka laki 9 hadi milioni moja na laki nne (million 1.4) ndani ya miezi 3 iliyopita,"alisema.

Alidokeza kwamba bado kuna Watanzania wengi ambao wanahitaji huduma za simu na internet na muhimu ni kulenga jamii ambazo bado hazijapata hizi huduma badala ya kugombania wateja sehemu moja.

Moyo, alisema Zantel sasa inazingatia kuongeza thamani kwa wateja wake pamoja na kuongeza huduma na bidhaa mpya sokoni.

Aliongeza kusema Zantel itawekeza kwenye maendeleo ya vijana na kuhakikisha maendeleo ya nchi yanapewa kipaumbele kwa kuwawezesha vijana. Moyo pia alisema Zantel ina nia ya kuongeza huduma zake vijijini kuwawezesha vijana wanaoishi vijijini kupata fursa ya kutumia huduma zitakazowasaidia kuendeleza maisha yao.

“Zantel kuungana na Etisalat inatupa nguvu kiuchumi haswa kwenye masuala ya kukunua vifaa na mitambo mipya ya kisasa pamoja na simu za kisasa kwani tunanunua kwa pamoja na sio kama Zantel peke yake. Unafuu huu ni faida kwa wateja wetu kwani wanapata simu nzuri na kwa bei nafuu wakati huo huo wakitumia mtandao wa kisasa na uliosambaa Tanzania nzima,” aliongeza Moyo.

Norman Moyo ni moja ya viongozi wapya waliotambulishwa kwa nia ya kuibadilisha kampuni ya Zantel. Akiwa na umri wa miaka 36 mkuu huyu wa kitengo cha biashara na ana uzoefu mkubwa katika sekta ya mawasiliano haswa kwenye kuyageuza makampuni kutoka kwenye hasara kuyafikisha kwenye faida.

Moyo ni mmoja ya wale waliobadilisha taswira ya masiliano nchini Zambia akiwa kama Mkurugenzi wa Masoko wa Celtel Zambia na baadaye kuwa Mkuu wa kitengo cha Masoko Celtel Nigeria na uteuzi wake ulibadilisha kampuni ya Celtel Nigeria hadi kuwa namba mbili kutoka wateja milioni 4.5 hadi wateja milioni 17 ndani ya miaka miwili na nusu.

No comments: