Thursday, May 29, 2008

Wanachama wafungia ndani uongozi Saccos


MGOGORO wa Chama cha Akiba na mikopo cha Lumumba Saccos Ltd umechukua sura mpya baada ya wanachama wake kuwafungia ofisini viongozi wa chama hicho, baadhi ya wanachama, Mrajisi wa ushirika mkoani Dar es Salaam na Mrajisi wa ushirika wa Wilaya ya Ilala.

Kitendo hicho kilitokea jana saa 4.45 wakati Mnajisi wa Mkoa aliyetambulika kwa jina moja la Mgoe na Mrajisi wa Ilala ambaye jina lake halikupatika walipokuwa wakizungumza na uongozi wa chama hicho.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na Mwananchi, wanachama hao walisema mazungumzo hayo yalitokana na maandamano yao kwa Mkuu wa Mkoa Abass Kandoro, juzi, kumuomba aingilie kati mgogoro wao ambao kiini chake ni kukosa imani na uongozi wa chama hicho.

Akizungumza kwa niaba ya wanachama wenzake, Emmanuel Mwambeta alisema maandamano hayo hayakuwawezesha kuonana na Kandoro ingawa waliahidiwa kuwa tatizo lao litapatiwa ufumbuzi.

Akizungumzia uamuzi wa kuwafungia viongozi na wawakilishi wao ofisini alisema ni kutokana na kukosa imani hali iliyotokana na kuzungushwa kwa muda mrefu bila kukopeshwa fedha au kukubaliwa kujiondoa katika chama hicho.

Dakika 40 baada ya viongozi hao kufungiwa ofisini, walijaribu kutoka nje kwa kupitia mlango wa ofisi ya pili ambayo inaingiliana na ofisi ya chama hicho hali iliyosababisha vurugu kubwa kiasi cha kuwafanya wamiliki wa ofisi hiyo ya pili kurudisha ndani.

No comments: