Friday, May 30, 2008

Waziri Mkuu asifu maandalizi ya Sullivan

WAZIRI MKUU Mizengo Pinda amesema ameridhishwa na maandalizi kwa ajili ya mkutano wa
nane wa kimataifa wa Leon Sullivan unaotarajiwa kufanyika Arusha kuanzia Jumatatu
ijayo.

“Tumekuwa na maandalizi ya muda mrefu, lakini kama Serikali ilibidi tufike kuona
hali halisi na kujiridhisha na jinsi kazi inavyokwenda… kwa kweli mambo yanakwenda
vizuri, kuna mabadiliko makubwa nimeyaona na mfano ni hapa AICC,” alisema Waziri
Mkuu.

Waziri Mkuu amesema hayo leo (Ijumaa, Mei 30, 2008) wakati akizungumza na waandishi
wa habari mara baada ya kumaliza kukagua ukumbi wa mikutano wa AICC ambako mkutano
huo utafanyika.

Kabla ya kukagua ukumbi huo, Waziri Mkuu alitembezwa katika Uwanja wa Ndege wa
Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) ambako wajumbe wa mkutano na wageni mashuhuri (VIPs)
watafikia kuanzia kesho (Jumamosi).

Alisisitiza haja ya kutowakawiza wageni hasa katika maeneo ya idara za Uhamiaji na
Forodha. “Sisemi kwamba muwaachie tu, hapana, nataka taratibu zifuatwe lakini zisiwe
kero…” alisisitiza.

Akiwa njiani kuelekea Arusha mjini, alikagua maeneo ya hoteli ya Ngurdoto ambako
wageni mashuhuri watafikia na ambako dhifa ya kitaifa itafanyika. Pia alifanya
mazungumzo na Kamati ya Maandalizi ya mkutano huo pamoja uongozi wa mkoa wa Arusha.

Waziri Mkuu amerejea Dar es Salaam leo jioni.
 
Ends

No comments: