Thursday, May 22, 2008

Afrika kusini hakukaliki sasa




MAELFU ya wahamiaji wameanza kuikimbia Afrika Kusini kutokana kushambuliwa na makundi ya raia wa nchi hiyo kwa siku kadhaa sasa. Mashambulizi hayo yamesababisha mauaji na inadaiwa mpaka Mei 22,2008 watu 42 ambao ni wageni wamepoteza maisha.
Msumbiji imeandaa mabasi maalumu kwa ajili ya kuwarejesha nyumbani raia wake na hadi Me1 21,2008 wananchi wake 9,000 wamekwisha kurejeshwa nyumbani wiki hii.
Baadhi ya raia wa Zimbabwe pia wanarejea kwao, wameona ni bora wakakumbane na vurugu za nchini mwao kuliko kuhatarisha maisha yao katika Afrika Kusini.
Wakati watu 42 wamekwisha kuuawa na wengine 15,000 wameomba hifadhi kukimbia mashambulio na vijana hao ambao wanawalaumu wageni kwa uhalifu na kusababisha ukosefu mkubwa wa kazi nchini Afrika Kusini.
Jeshi la nchi hiyo linatumika kusaidia kukabili vurugu hizo – ikiwa ni kwa mara ya kwanza tangu kumalizika kwa utawala wa kibaguzi mwaka 1994. Lakini polisi wa Johannesburg ambako vurugu hizo zilianzia wamesema hivi sasa hali ni tulivu kwa kiasi fulani.
Polisi walitumia risasi za mpira na mabomu ya kutoa machozi kuyatawanya makundi ya vijana waliokuwa wanafanya vurugu. Raia wa Zimbabwe wapatao milioni tatu wanaaminika wako Afrika Kusini hivi sasa baada ya kukimbia njaa na vurugu nchini mwao.

No comments: