Thursday, May 29, 2008

Polisi wanaodiwa kushirikiana na Zombe watajwa



WATUHUMIWA wawili katika kesi ya mauaji ya wafanyabiashara wa madini waliouwa Januari 14, 2006 jijini Dar es Salaam wakidhaniwa kuwa ni majambazi jana wametambuliwa kuwa ni miongoni mwa askari polisi waliohusika kuwakamata marehemu hao kabla ya kuuawa.

Shahidi wa sita katika kesi hiyo, Mjatta Kayamba mkazi wa Sinza C, Palestina, alimtambua mtuhumiwa namba tatu ASP Ahmed Makele na mtuhumiwa wa tano WP.4593 Jane Andrew kwamba walihusika katika tukio hilo.

Akitoa ushahidi huo mbele ya Jaji Salum Masatti wa Mahakama Kuu ya Tanzania, anayesikiliza kesi hiyo, shahidi huyo alidai askari hao ni miongoni mwa askari watatu waliofika Sinza Palestina karibu na nyumbani kwa Mathew Ngonyani ambako wafanyabiashara hao walikuwa wamekwenda.

Kayamba alidai kuwa, siku hiyo akiwa nyumbani kwake, aliwaona wafanyabiashara hao wakielekea nyumbani kwa Ngonyani wakiwa na gari dogo na kusalimiana na mke wa Ngonyani na muda mfupi baadaye wakati wafanyabiashara hao wanataka kuondoka ilifika gari aina ya Toyota Stout na kuzuia gari ya wafanyabiashara hao kuondoka kwenye eneo hilo.

No comments: