Thursday, April 17, 2014

Wakala wa huduma za ajira (TaESA) imefanikiwa kuanzisha Ofisi za Kanda katika Mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Mwanza na Arusha ili kusogeza huduma zake karibu na wananchi

Msemaji wa Wakala wa Huduma za ajira (TaESA) bw. Peter Ugata (katikati) akiwaeleza waandishi wa habari jana jijini Dar es salaam kuhusu mafanikio yaliyofikiwa na wakala huo ikiwemo kuanzisha ofisi za Kanda katika Mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Mwanza na Arusha ili kusogeza huduma kwa wananchi. Kulia ni Mratibu wa Huduma za Ajira toka wakala huo Bw. Joseph Haule na Kushoto ni Afisa Habari wa Idara ya Habari Maelezo Bi Fatma Salum.
Baadhi ya Waandishi wa Habari wakifuatilia mkutano wa Wakala wa Huduma za ajira (TaESA) uliofanyika katika ukumbi wa Idara ya Habari Maelezo  jijini Dar es salaam leo.Picha na Frank Mvungi, MAELEZO
--
Frank Mvungi-Maelezo
Wakala wa huduma za ajira (TaESA) imefanikiwa kuanzisha Ofisi za Kanda katika Mikoa ya Dar es salaam, Dodoma, Mwanza na Arusha ili kusogeza huduma zake karibu na wananchi.
Hayo yamesemwa na Msemaji wa wakala wa Huduma za ajira Bw. Peter Ugata wakati wa mkutano na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam.

Akifafanua Ugata amesema kuwa wakala imefanikiwa kuanzisha ofisi katika mikoa hiyo ikiwa ni moja ya hatua za kuboresha huduma zinazotolewa na wakala huo hapa nchini.
Akieleza zaidi Ugata alisema kuwa wakala huo umeshawahudumia jumla ya wateja 14,608 kati yao wanaotafuta kazi ni 13,531 waajiri 993 na wakala binafsi zilikuwa 84.

Kwa upande wa kusajili fursa za kazi Ugata alisema wakala umesajili fursa za kazi 3,143 kwa kutembelea waajiri 993 katika Mikoa ya Shinyanga, Kagera, Mara, Mwanza, Singida, Tabora, Iringa, Morogoro, Lindi, Arusha, Kilimanjaro na Mtwara.

Katika kuboresha huduma zake, Ugata amesema kuwa wakala uko katika hatua za awali za kuweka mfumo wa kiteknolojia utakaowezesha kukusanya na kusambaza taarifa za soko la ajira.

Katika hatua nyingine Ugata amesema wakala kupitia kitengo cha kuwaunganisha watafutakazi 2,614na waajiri nje ya nchi za nje kama Ujerumani, Brazil, China, Saudi Arabia, Denmark, India na Oman.

Katika kuhamasisha wananchi kutumia huduma za wakala huo, Ugata amesema kuwa wakala umeweka utaratibu madhubuti wa kuratibu na kusimamia uunganishaji wa watanzania kwenye soko la ajira nje ya nchi ili wapate kazi zenye staha na kuepukana na biashara haramu ya usafirishaji watu (Human Traffiking).

Wakala wa huduma za Ajira (TaESA) unatekeleza Sera ya Taifa ya ajira ya mwaka 2008 na Sheria ya kukuza Ajira Na. 9 ya mwaka 1999 na katika hatua ya kukidhi matakwa ya Azimio NA.88 la mwaka 1948 la shirika la kazi Duniani (ILO) ambalo Tanzania imeridhia.

No comments: