Wednesday, January 27, 2010

Wanajeshi wanaodaiwa kumuua mtoto wa Fundikira kizimbani



ASKARI wawili wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) jana walipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kujibu tuhuma za mauaji ya mtoto wa mwanasiasa maarufu, Chifu Abdallah Fundikira.

Watu hao, Rhoda Robert, 42, wa cheo cha sajenti mwenye namba MTM 1900 kutoka kambi ya JKT Mbweni na MT 75854 Koplo Ally Ngumbe, 37, wa kambi ya JWTZ Kunduchi, wanakabiliwa na mashtaka ya kumuua Swetu Fundikira, 45.

Akisoma hati ya mashitaka mbele ya Hakimu Mkazi Geni-Vitus Dudu, wakili wa serikali, Monica Mbogo alidai kuwa washtakiwa walifanya mauaji hayo Januari 23, mwaka huu, majira ya saa 7:30 usiku kwenye Barabara ya Mwinjuma wilayani Kinondoni.

Washtakiwa hao hawakutakiwa kujibu chochote kwa sababu shtaka hilo linalowakabili ni moja ya mashtaka ambayo Mahakama ya Kisutu haina uwezo wa kuyasikiliza bali Mahakama Kuu.

Hakimu Dudu aliamuru askari hao walirudishwe rumande kwa kuwa shtaka hilo lao halina dhamana na akaiahirisha kesi hiyo hadi Februari 10 itakapotajwa tena baada ya upande wa mashtaka kudai upelelezi bado haujakamilika.

Askari hao wanadaiwa kumuua Swetu kwa kumpiga wakiwa pamoja na mwanajeshi mwingine mmoja baada ya kutokea ugomvi wa barabarani uliotokana na askari hao kudai kuwa walifanyiwa fujo na kutukanwa.

Swetu alifariki dunia Jumapili usiku akiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kutokana na kipigo hicho. Imeandikwa na Tausi Ally

No comments: