Tuesday, January 05, 2010

Jacob Zuma Rais aoa mke mpya wa 5






BAADA ya uvumi mkubwa uliopingwa na maofisa kadhaa wa serikali na familia ya Rais Jacob Zuma wa Afrika Kusini, jana amefunga ndoa rasmi na mke mpya wa tano huku mipango ikiwa mbioni kuoa mke wa sita.

Jana Rais huyo alikuwa akifunga ndoa na Thobeka Madiba. Kaka wa Rais Zuma, Inkosi Bhekumuzi Zuma aliweka wazi kuwa ‘mipango ya ndoa ya sita’ imeanza kwani mchumba mwingine wa Rais Zuma, Gloria Bongi Ngema kutoka Durban, ameshawasilisha umbondo kwa familia ya Zuma Jumatatu iliyopita.

Umbondo ni zawadi za kitamaduni kwa ajili ya familia ya mume mtarajiwa ambayo hutolewa na mke mtarajiwa akionesha ishara kuwa lobola (mahari) ya kumuoa imeshalipwa yote. Kwa maana hiyo, Rais Zuma ameshakamilisha mahari ya kumuoa mke wa sita.

Wakati katika tamaduni zingine zilizoathiriwa na tamaduni za Kimagharibi jamii ingekuja juu kupinga harusi hizo, wakazi wa eneo la ukoo analoishi Rais Zuma la Nxamalala wameelezea furaha yao kwa uamuzi huo wa Rais.

Richard Zuma, ambaye si ndugu wa karibu wa Rais Zuma amesema matayarisho kwa ajili ya harusi ya ‘kufungua mwaka’ yalianza muda mrefu tangu Desemba 20 na kuongeza kuwa kitendo cha jamii ya eneo hilo kutokuzungumzia matayarisho hayo, kinaonesha furaha waliyonayo kwa Rais Zuma. kwa taarifa za kina hebu soma hapa

1 comment:

Masangu Matondo Nzuzullima (MMN) said...

Anadumisha mila na utamaduni wa Mwafrika huyu. Kuna nini cha kushangaza hapa? Waisilamu wakioa wake wengi mbona hatushangai?

Kule Usukumani (na naamini pia katika makabila mengi) bado ni rukhsa kuoa wake wengi na kijijini kwetu kuna jamaa wenye wake wawili, watatu, wanne, watano na hata sita.

Hata hao wasio na wake wengi - wana nyumba ndogo Ilala, Temeke na Kinondoni? Si ni kitu kile kile tu au?