Friday, January 29, 2010

Mkenya ainusa Man City



KIUNGO wa Kenya, McDonald Mariga anakaribia kuwa Mkenya wa kwanza kucheza Ligi Kuu ya England baada ya klabu ya Manchester City kuamua kumnunua kutokana na juhudi zao za kumpata Fernando Gago wa Real Madrid kugonga mwamba.
Inter Milan pia imekuwa ikimfuatilia mchezaji huyo wa kimataifa wa Kenya anayechezea Parma ya Italia, lakini inaonekana imeamua kuachana naye baada ya kumpata Manuel Fernando kwa mkopo kutoka Valencia.
Gazeti la Daily Mail limeripoti jana kuwa Man City iko tayari kulipa kitita cha Pauni 6 milioni kumnunua Mariga na inaweza inaweza kumuachia Valeri Bojinov ikiwa ni sehemu ya mpango huo.
Kocha Harry Redknapp alijaribu kumnunua Mariga kutoka klabu ya Helsingborgs ya Sweden wakati akifundisha Portsmouth miaka mitatu iliyopita, lakini kibali cha kazi kilimkwamisha.
Lakini hivi sasa kiungo huyo wa Parma amejichimbia kwenye kikosi cha kwanza, akivutia mashabiki wengi tangu ajiunge na klabu hiyo mwaka 2007.

No comments: