Wednesday, January 06, 2010

Bandari ya Zanzibar leo hii




Kwa wengi wasiojua bandari ya Zanzibar ilikuwa na umuhimu mkubwa katika eneo hili la Bahari ya Hindi kwa kuwa ilikuwa ni kituo kikubwa cha kutia nanga meli zilizokuwa zikitoka chini ya Afrika kutokea Marekani na juu ya Afrika kutoka Asia na hata Ulaya.

Zanzibar ilikuwa ikitawala ukanda wa pwani ya Afrika Mashariki kutoka chini ya Somalia mpaka Sofala, Mozambique, ilihitaji
bandari yenye uwezo na haiba.Mwaka 1892 ilitangazwa nia ya kuifanya Zanzibar

Bandari Huru wazo ambalo halikuwahi kutimizwa kikamilifu na hata baada ya nia hiyo kusisitizwa upya katika miaka ya hivi karibuni basi bado imekuwa ni ndoto.

Kwa maumbile yake ya visiwa bandari ina nafasi maalum katika uchumi, hilo halina shaka yoyote ile. Na kwa hivyo uhai na uzima wa bandari unamgusa kila mtu hapa kwetu.

Ndio maana bandari ilipokuwa inaugua uchumi wa Zanzibar na watu wake walikuwa wanaugua. Ndio maana wakati mivutano ya kisiasa ilipokuwa ikirindima na kukawiza ufadhili wa mradi huo uchumi wa Zanzibar uliumwa nawatu wake waliumwa.
Na pia wakati mvutano uliotokea kuhusu aina ya ujenzi wa bandari hiyo, uchumi wa Zanzibar uliumwa na watu wake waliugua.

Lakini wengi tumekuwa tunajiuliza katika mazingira tuliyonayo au ambayo tunalazimishwa kuishi nayo ni rahisi kiasi gani ujenzi mpya wa bandari hiyo kuwa na faida kwa uchumi wa Zanzibar? Hapa ni maana mbili. Moja ni ile ya mfumo mzima unaozunguka suala la faida ya ushuru unaoweza kutokana na harakati za bandari hiyo kuingiza na kutoa bidhaa, ambalo hili liko nje ya uwezo au utawala wa Serikali ya Zanzibar kwa upande fulani.

Na maana ya pili ni uwezo ulio ndani wa menejimenti ya bandari hiyo kusimamia na kuwa tayari kivifaa na kitaalamu ili kazi za bandari hiyo ziwe na natija ambayo umma wa Kizanzibari unatarajia kimapato na kiajira? Kwa sasa bandari ya Zanzibar inafanya kazi katika hali ya ushindani mkubwa. Ushindani nje ya Tanzania dhidi ya bandari ya Mombasa na upinzani ndani ya Tanzania dhidi ya bandari ya Tanga lakini hasa Dar es Salaam na hatua zikianza kuchukuliwa kuiwezesha zaidi ile ya Mtwara.

No comments: