Thursday, June 25, 2015

TAHADHARI YA UGONJWA WA NIMONIA INAYOTOKANA NA CORONA VIRUS

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA AFYA NA USTAWI WA JAMII
index
TAARIFA KWA UMMA.
TAHADHARI YA UGONJWA WA NIMONIA INAYOTOKANA NA CORONA VIRUS
…………………………………………………..
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, inapenda kutoa tahadhari ya ugonjwa wa nimonia inayotokana na kirusi kiitwacho Corona virus. Mnamo tarehe 21 Mei 2015, Wizara ilipokea taarifa kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) juu ya kusambaa kwa kasi kwa ugonjwa wa Nimonia unaosababishwa na kirusi cha “Coronavirus”, Korea ya Kusini.
Ugonjwa huu unaenezwa na kirusi kiitwacho “Middle East Respiratory Syndrome Coronavirus (MERS Cov).” Dalili kuu za ugonjwa huu ni homa kali, kukohoa na kushindwa kupumua kwa ghafla, na hatimaye kupata Nimonia. Dalili nyingine ambazo zinaweza kutokea ni pamoja na kupata maumivu makali ya tumbo pamoja na kuharisha. Kipindi kati ya kupata maambukizi mpaka kuonekana kwa dalili za ugonjwa ni kati ya siku 2 hadi 10. Ugonjwa huu hutibiwa kufuatana na dalili zilizojitokeza. Mpaka sasa hakuna chanjo maalum kwa ajili ya ugonjwa huu.
Virusi hivi, kutokana na tafiti zinazoendelea hubebwa na wanyama hususan ngamia na tafiti hizi zimeonyesha uwepo wa virusi hivi kwenye ngamia katika nchi za Egypt, Oman, Qatar na Saudi Arabia. Mara mgonjwa apatapo ugonjwa huu, uambukizo kwenda kwa mtu mmoja hutokea iwapo mtu huyu atakuwa karibu na mgonjwa aliyethibitishwa kuwa na ugonjwa huu na kugusa majiimaji au makamasi hasa wakati wa kukohoa au kupiga chafya. Vilevile uambukizo huweza kutokea iwapo mtu akigusa mazingira ambayo yamechafuliwa na majimaji au makamasi ya mgonjwa aliyedhibitishwa na ugonjwa huu.
Ugonjwa wa Corona virus uligundulika kwa mara ya kwanza mwezi Septemba 2012 katika nchi za Mashariki ya kati huko Saudi Arabia. Ugonjwa huo umeendelea kusambaa katika nchi za Mashariki ya kati zikiwemo za Jordan, Qatar, na Falme za Kiarabu (UAE). Katika bara la Ulaya, ugonjwa huu umethibitishwa kutokea nchi za Ujerumani, Ufaransa, na Uingereza na barani katika nchi ya Tunisia. Ugonjwa huu umeendelea kuwepo kwenye nchi hizi kwa kiwango kidogo kuanzia mwaka 2012 hadi Aprili 2015.
Ongezeko la ugonjwa huu limejitokeza zaidi kuanzia tarehe 20 Mei, 2015 katika nchi ya Jamhuri ya Korea. Hadi tarehe 20 Juni, 2015, watu 167 walikuwa wamethibitishwa kuwa na ugonjwa huo wa nimonia ya Corona Virus na 24 kupoteza maisha. Vile vile nchi za Thailand na China kumekuwa na mgojwa mmoja kila nchi.
Hadi sasa hakuna mgonjwa yoyote aliyehisiwa au kuthibitishwa kuwa na virusi vya Corona virus hapa nchini. Kwa kuwa magonjwa hayatambui mipaka ya nchi ni vyema tuchukue tahadhari dhidhi ya Ugonjwa huu.
Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imeandaa mikakati ya kuzuia ugonjwa huu usiingie hapa nchini ikiwa ni pamoja na;
• Kuongeza kasi ya ufuatiliaji wa magonjwa (Surveillance) hususan katika vituo vitano maalum vilivyopo nchini vinavyofanya ufuatiliaji wa magojnwa ya neumonía (Influenza sentinel surveillance sites).
• Kuongeza kasi ya ufuatiliaji kwa vituo vya kutolea huduma kote nchini. Aidha Wizara imeagiza kupitia waganga wakuu wa mikoa kutoa taarifa /ongezeko la wagonjwa watakaoonyesha dalili za ugonjwa huo hususan kwa wagonjwa ambao wamesafiri kwenye nchi ambazo zina ugojnjwa huu. Ainisho sanifu (Standard case Definition) imetolewa kusaidia mtaalamu wa afya kuweza kutambua ugonjwa huu. Aidha kasi hii ya ufuatiliaji inaangalia iwapo kuna ongezeko la Nimonia kali au mafua kulinganisha na majira ya wakati huu kwa miaka mingine.
• Kuongeza kasi ya ufuatiliaji wa ugonjwa huu maeneo ya mipakani hususan kwa wasafiri watokao nje ya nchi hususani watokao nchi za Mashariki ya Kati, pamoja na Bara ya Ulaya na Afrika, kwa kutumia mifumo ile ile iliyowekwa kwa wagonjwa ya kuambukiza kama Ebola ambayo yaweza kuingia nchini kupitia mipaka yetu. Ufuatiliaji huu hufanyika bila kusababisha usumbufu usio wa lazima kwa wasafiri.
• Kuendelea na upimaji wa sampuli zinazohisiwa kuwa na ugonjwa huu. Aidha Maabara ya taifa imejengewa uwezo wa kupima virusi vya Corona virusi. Sampuli zilizopimwa kuanzia April mpaka Juni 2015 zimethibitisha kuwa hakuna ugonjwa huo hapa nchini.
• Kutoa taarifa ya tahadhari ya ugonjwa huu kupitia kwa Waganga Wakuu wote wa Mikoa na Wilaya kwa Tanzania bara. Aidha taarifa hii pia imejumuisha namna mgonjwa anavyoweza kutambuliwa (Ainisho la Ugonjwa), “Fact sheet” ya ugonjwa, Mwongozo kwa watumishi wa afya wa namna ya kuchukua sampuli ikiwa ni pamoja na vipeperushi vinavyoelezea jinsi ya kujikinga na maambukizi ya ugonjwa huu.
• Kutoa elimu wa jamii kupitia kwa Wataalamu wa Afya katika Mikoa, Wilaya na maeneo ya mipakani kuhusu dalili za ugonjwa huu na jinsi ya kujikinga na maambukizi ili endapo ugonjwa huo utatokea uweze kutolewa taarifa mapema.
• Kutoa mafunzo kwa watumishi wa afya na mipakani wa namna ya kutambua na kujikinga dhidi ya maambukizo ya ugonjwa huu pamoja na uchukuaji wa sampuli iwapo mgonjwa atapatikana huku wakizingatia kanuni za usafi (Infection, Prevention and Control)
• Wizara inasisitiza kuwa hakuna vikwazo vyovyote vilivyowekwa kwa ajili kwa wasafiri watakaokwenda au kurudi katika maeneo tajwa yaliyothibitishwa kuwa na ugonjwa huu.
Hitimisho
Wananchi wanashauriwa kutokuwa na hofu kwani mpaka sasa hakuna mgonjwa yeyote aliyeripotiwa nchini.
Ugonjwa huu unaambukizwa kwa njia ya hewa iwapo mgonjwa atokohoa au kupiga chafya bila kujikinga au pia kugusa sehemu zenye ugonjwa huo na kujigusa mdomomi au puani. Kwa kuzingatia hali hiyo, wizara inapenda kutoa tahadhari kwa wananchi juu ya umuhimu wa kunawa mikono vizuri kwa sabuni na maji mara kwa mara na pia kuzuia mdomo na pua kwa kitambaa au karatasi laini (tissue paper) wakati unapokohoa au kupiga chafya.
Mpaka sasa hakuna kizuizi cha kusafiri kutoka nchi moja hadi nyingine. Hata hivyo inashauriwa kwamba mtu yeyote anayesafiri kwenda Mashariki ya Mbali na nchi za Asia afahamu kuwa kuna hatari ya ugonjwa huu na kwamba anatakiwa atoe taarifa mapema kwenye taasisi za huduma za afya iwapo ataona dalili kama hizi wakati akiwa safarini au wakati amewasili toka nchi ambazo zina ugonjwa huu.
Vilevile, wananchi wanashauriwa kutoa taarifa kwenye kituo cha kutolea huduma za afya kilicho karibu mara watakapoona mgonjwa yeyote atakayehisiwa kuwa na dalili za ugonjwa huu.
Imetolewa na;
Kitengo cha Mawasiliano Serikali – Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii
Juni 25,2015

No comments: