TUME ya Kudhibiti UKIMWI nchini (TACAIDS) imesema mkoa wa Njombe unaongoza kwa kuwa na maambukizi makubwa ya Virusi vya UKIMWI kwa asilimia 14.8 ikifuatiwa na Iringa kwa asilimia 9.1.

Mkoa wa Mbeya unashika nafasi ya nne kwa asilimia tisa ukifuatiwa na Ruvuma (7.2), Shinyanga (7.4), Dar es Salaam (6.9) Rukwa (6.2), Katavi (5.9), Pwani (5.9),Tabora (5.1), Kagera (4.8) na Geita (4.7).

Msemaji wa TACAIDS, Glory Mziray alisema hayo jana Dar es Salaam na wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Mikoa mingine na viwango vyake ni Mara (4.5), Mwanza (4.2),Mtwara (4.10), Kilimanjaro (3.8), Kigoma (3.4), Simiyu (3.6), Morogoro (3.8), Singida (3.3), Dodoma (2.9), Manyara (1.5), Lindi (2.9), Tanga (2.4), Unguja (1.9) na Pemba (0.3).

Alisema takwimu hizo zinatokana na utafiti uliofanyika mwaka juzi hadi mwaka jana. Kutokana na matokeo hayo, alisema maambukizi ya UKIMWI yamepungua kwa kasi ndogo.

Alisema watanzania walioonesha kuwa na ufahamu sahihi wa elimu kuhusu Virusi vya ukimwi na UKIMWI wanafikia asilimia 60 jambo linalosababisha kuwepo mwamko mdogo wa kubadili tabia.

Kuhusu tohara kwa wanaume endapo inapunguza maambukizi ya UKIMWI alisema inapunguza kwa asilimia 60 na kusisitiza kuwa ipo haja kutoa elimu zaidi juuya uelewa wa ugonjwa huo.