Wednesday, July 24, 2013

RAIS KIKWETE ATOA MAELEKEZO KUHUSU KODI YA SIMU ZA MKONONI

Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika picha ya pamoja na maofisa waandamizi wa Wizara ya pamoja na wajumbe wa Chama cha  Makampuni ya Simu za mkononi alipokutana nao kwa mazungumzo Ikulu jijini Dar es Salaam leo Julai 23, 2013(PICHA NA IKULU)
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameagiza Wizara za Serikali zinahusika na kodi na mawasiliano pamoja na makampuni ya simu za mikononi nchini kukutana mara moja kutafuta jinsi gani ya kumaliza mvutano wa kodi mpya ya kadi za simu hizo za mikononi.
Rais kikwete ametoa maelekezo hayo jioni ya leo, Jumanne Julai 23, 2013 wakati alipokutana na viongozi wa Wizara ya Fedha, Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia na wawakilishi wa makampuni ya simu ya TTCL, Airtel, Vodacom, Tigo na Zantel katika kikao cha pamoja kilichofanyika Ikulu, Dar es Salaam.
Rais Kikwete amesema kuwa lengo kuu la mkutano huo wa pamoja kati ya Wizara hizo za Serikali na makampuni ya simu yawe ya kupendekeza jinsi gani ya kuziba pengo la Sh. Bilioni 178 ambazo zitapotea katika Bajeti iwapo kodi hiyo kwa kadi za kuongelea za simu za mikononi italazimika kufutwa na Serikali kupitia marekebisho kwenye Muswada wa Fedha wa Bajeti ya Mwaka 2013/2014.
Rais Kikwete amewaambia wawakilishi wa pande hizo mbili kuwa huwezi tena kuifuta moja kwa moja kodi hiyo bila kutafuta njia nyingine za kupata fedha za kujaza pengo hilo la Sh. Bilioni 178 ambazo tayari Bunge limezipangia matumizi.
“Nawaombeni kaeni pamoja, wekeni bongo zenu pamoja, wekeni akili yenu pamoja tutafute namna gani tunaweza kujaza pengo hili la Sh. Bilioni 178 endapo tutakubaliana kuwa kodi hii inawabebesha wananchi mzigo mzito na kuwa pengine menejimenti ya kodi yenyewe ni ngumu,” Rais Kikwete amewaambia wawakilisho hao.
Katika Bajeti ya Serikali ya mwaka 2013/2014, Serikali imeweka kodi ya Sh. 1,000/= kwa mwezi kwa kila mtumiaji simu kwa ajili ya kufanya mawasiliano kwa kutumia simu ya mkononi.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
23 Julai, 2013

No comments: