Monday, February 04, 2008

Wabunge wakataa semina ya Karamagi

WABUNGE wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania jana walikataa kuendelea na semina iliyoandaliwa na Wizara ya Nishati na Madini kwa ajili ya kuwaelimisha kuhusu mswaada wa Sheria za Umeme na Biashara ya Mafuta ya Petroli na kutaka waletewe kwanza ripoti ya Kamati ya Richmond waijadili kabla ya kupitisha mswada huo.

Sambamba na hilo wabunge hao wamesema hawana imani na wizara hiyo pamoja na Shirika lake la Umeme (Tanesco) kwa kuwa taasisi hizo zimejaa uchafu na kwamba hawawezi kujadili masuala ya mikataba mengine mpaka wajisafishe.

Semina hiyo iliyokuwa chini ya uenyekiti wa Dk Harrison Mwakyembe, ilianza saa tano asubuhi kwa Waziri wa Nishati na Madini kufungua semina hiyo kisha wakuu wa idara mbalimbali za Tanesco kutoa maelezo kuhusu umuhimu wa kuwapo kwa sheria hiyo.

Dosari ilianza kujitokeza mapema mara tu baada ya wakuu hao wa idara wakiongozwa na Kamishina wa Petroli, Bashiri Mrindoko, kutoa maelezo, ambapo Naibu Spika, Anna Makinda alisimama na kuomba muongozo wa mwenyekiti na kusema kuwa maelezo hayo hayatoshelezi na kwamba hawakuelewa chochote wakati wanapewa maelezo hayo.

"Muheshimiwa Mwenyekiti naomba muongozo wako, Mimi sielewi kabisa na mbaya zaidi hatujaelimishwa chochote kuhusu sheria hii, tulivyoingia humu ndani na mpaka tunatoka, hakuna tofauti yoyote, watendaji wameshindwa kutuelimisha umuhimu na maudhui ya sheria hii, ili tupate kwenda kuwaelimisha wananchi wetu majimboni, ilitakiwa kusema sheria ya zamani inashida gani na hii mpya ina manufaa gaini kwa wananchi," alisema Makinda.

Kufutia kauli hiyo, Waziri Karamagi ilibidi kutoa ufafanuzi mwenyewe kuhusu umuhimu wa sheria hiyo ambapo pamoja na mambo mengine alisema kuwa sheria hiyo itaondoa ukiritimba na kutoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza katika sekta ya umeme nchini.

Hata hivyo mara baada ya kutoa ufafanuzi huo Mbunge wa Vunjo (CCM), Aloyce Kimaro alisimama na kuomba tena muongozo wa mwenyekiti na kutaka semina hiyo isimamishe mpaka pale Bunge litakapopata ripoti ya kamati ya Richmond na kuijadili ndipo mikataba hiyo ifikishwe Bungeni na kwamba yeye mwenyewe hana imani na wizara hiyo pamoja na watendaji wake.

Hata hivyo Dk Mwakyembe alikataa ombi hilo na kusema: "Wabunge kama mnavyeoelewa semina haina haina uwezo wa kusimamisha shughuli za bunge, nawaomba wabunge wenzangu tukubali kupata elimu kwanza kama ilivyo desturi yetu, tuache taratibu nyingine zifuate suala la kusimamisha miswada tuiachia Bunge".

Mbunge wa Same Mashariki, Anna Kilango naye alisimama na kusema wabunge wamechoka kuonekana wajinga mbele ya wananchi kwa kukubali kupitisha mambo bila kufikiri na kubambikiwa na kwamba hata wakikaa hapo kwa zaidi ya siku nne hawatakubali muswada huo kujadiliwa.

No comments: