Friday, February 22, 2008

Lowassa kuwasha moto Monduli

WAZIRI Mkuu aliyejiuzulu kwa kashfa ya Richmond, Edward Lowassa kesho anatarajiwa kurejea jimboni kwake Monduli ambako atahutubia wapiga kura wake na kuwaeleza hali iliyosababisha akachukua uamuzi wa kujiuzulu.

Kwa mujibu wa habari kutoka kwa viongozi mbalimbali wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa wilaya ya Monduli Lowassa anatarajiwa kuwasili katika uwanja wa ndege wa Arusha uliopo Kisongo saa tatu asubuhi.

Mara baada ya kutua muda huo katika uwanja huo na kupokewa na vikundi vya ngoma, msafara wa magari ya waliokuja kumpokea utakwenda katika jimbo lake.

Habari kutoka katika vikao vya chama wilayani Monduli zilisema kuwa uamuzi wa kumpokea Lowassa ambaye ni mbunge wa jimbo hilo kwa zaidi ya miaka 15 uliamuriwa katika vikao hivyo na mbunge huyo kujulishwa na siyo uamuzi wake.

“Sisi ndio tulioamua katika vikao kumpokea kwa maandamano ya magari na hata kwa miguu kwani amefanya uamuzi wa kidemkrasia ambao ni viongozi wachache tu wa kiafrika wenye moyo huo,’’ alisema kiongozi mmoja wa CCM.

Inaaminika Lowassa atatumia muda wa wiki nzima kufanya mikutano ya hadhara katika jimbo hilo kuelezea mstakabali mzima kwa wapiga kura wake ambao wengi wao bado hawajafahamu kilichofanya achukue uamuzi wa kujiuzulu Uwaziri mkuu.

Katibu wa CCM wa wilaya ya Monduli Allan Kingazi hakuweza kupatikana kuelezea hali halisi ya mapokezi hayo.

No comments: