Saturday, October 06, 2007

JK kuwasili Dar kesho



Rais Jakaya Kikwete leo anatarajiwa kurejea nyumbani kutoka ziara yake ya wiki tatu nchini Marekani, ambako pamoja na mambo mengine alihudhuria Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.

Kwa mujibu wa taarifa ya Ikulu iliyotolewa jijini Dar es Salaam jana, Rais Kikwete atawasili Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere mchana kwa ndege ya Shirika la Ndege la Emirates.

Taarifa hiyo ilisema wakati wa ziara yake, iliyoanza Septemba 15, amefanya mambo mengi yenye manufaa kwa nchi katika nyanja za siasa, uwekezaji, utalii, madini, michezo, biashara, elimu na utamaduni.

Miongoni mwa mafanikio hayo ni pamoja na kuzidisha kwa uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Marekani ambako taifa hilo kubwa limeahidi kusaidia mafunzo katika maeneo ya kijeshi.

Katika eneo la uwekezaji, makampuni kadhaa yameonyesha nia ya kujenga viwanda vya mbolea nchini na miradi mingine. Miongoni mwa makampuni makubwa yaliyoihakikishia Tanzania fedha za kuwekeza katika uchumi ni JP Morgan, Merrill Lynch, Tegris na Gibraltar Properties,

Wakati wa ziara yake, rais alizindua matangazo ya vivutio vya utalii wa Tanzania katika televisheni ya kimataifa ya CNN.

Makampuni kadhaa ya Marekani pia yamekubali kuwekeza katika utalii wa Tanzania miongoni mwao ikiwemo kampuni maarufu ya mahoteli ya Global Hyatt Corporation, ambayo imekubali kuja Tanzania na kuangalia maeneo ya kujenga mahoteli.

No comments: