Tuesday, October 30, 2007

Jenerali Ulimwengu ajiengua Habari Corporation

ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kampuni ya Habari Corperation, Jenerali Ulimwengu amejitoa katika kampuni hiyo na kuanzisha gazeti lake lingine.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Ulimwengu alisema wamejitoa katika kampuni hiyo kwa sababu za kibiashara na kwamba gazeti hilo la wiki litajulikana kama ‘Raia Mwema’.

“Sababu za kibishara zimefanya kujitoa Habari Corporation,” alisema Ulimwengu.

Alisema gazeti hilo litaanza kutoka kesho na litaendeshwa na kusimamiwa na waandishi, John Bwire, Johnson Mbwambo, Mbaraka Islam, Francis Chirwa na Shaban Kanua.

“Gazeti hili halina uhusiano wowote na Habari Corporation, tumeuza hisa zetu na tumeona tuanzishe gazeti lingine, nguvu zetu zote zitaelekezwa katika gazeti hilo na tutakuwa makini,” alisema Ulimwengu.

Alisema gazeti hilo likizingatia maadili ya taaluma ya uandishi wa habari na kwamba litasomwa Tanzania na Afrika Mashariki yote.

Ulimwengu alisema pamoja na Tanzania kupiga hatua kubwa katika sekta ya habari, bado mchango unahitajika ili kuendeleza sekta hiyo nchini.

Alitoa wito kwa vijana nchini kujitokeza na kuanzisha vyombo vya habari kwani bado kuna nafasi ya kuueleza umma mambo mbalimbali yanayotokea nchini na duniani kwa ujumla.

Ulimwengu alisema gazeti hilo, litakuwa likitoka mara moja kila wiki na litakuwa likiandika habari za kisiasa na michezo.

Alisema kuwa gazeti hilo halijaanzishwa kwaajili ya kuishambulia serikali na kwamba litakuwa likiandika makala na habari za kuisifia au kuikoa serikali pale inapostahili.

“Tunataka tutoe mchango wetu katika jamii kwaajili ya maendeleo ya nchi yangu na wala hatuanzishi ‘Raia Mwema’ ili kuziba mapengo ya uandishi,” alisema Ulimwengu.

2 comments:

Simon Kitururu said...

Tunasubiri kwa hamu mambo ya uhakika katika gazeti hili jipya.

Unknown said...

Muheshimiwa leo nimepita hapaa''
kazi nzuri.. fanya juu chini ushushe dondoo za kurasa za gazeti
hiii mwanana..
kwani kwa hili tu muheshimiwa' nakupa Tano.
Admin.
www.Haki-hakingowi.blogspot.com