Friday, September 16, 2016

Vijana nchini wahimizwa kuunga mkono kampeni ya Uchumi wa Kijani


Mkutano Vijana na Uchumi wa Kijani
Baadhi ya picha kutoka katika mkutano huo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika lisilo la Kiserikali la Raleigh Tanzania, Bw Alistar Mackay akizungumza na washiriki wa mkutano 


Washiriki wa mkutano huo 
Wawakilishi wa taasisi na ofisi za serikali 
Mgeni Rasmi akizungumza na waandishi wa habari 

Ms Clara Makenya kutoka United Nations Environment Programme akizungumzia uchumi wa kijani katika mkutano huo.

Vijana nchini Tanzania wahimizwa kujiunga na kampeni ya Vijana kwa Maendeleo ya Kijani ili kulinda mazingira kwa kuyafanya endelevu sambamba na kujiiinua kiuchumi.

Hayo yalibainishwa na Afisa Mawasiliano wa shirika la kimataifa la Raleigh Tanzania Bw. Kennedy Mmari wakati wa hafla ya uzinduzi wa Kampeni ya Uchumi wa Kijani kwa Vijana iliyofanyika kwatika ukumbi wa British Council.

Bwana Mmari alisema kuwa wao kama shirika linalojihusisha na vijana wamekuja na kampeni hii ya kitaifa kwakua wanaamini uwezo walionao vijana katika kuleta mabadiliko endapo watapewa nafasi.

“Sisi kama vijana tunahitaji sana maendeleo ya kiuchumi ila lazima maendeleo hayo yalinde mazingira yetu hivyo basi tunahitaji uchumi wa kijani, uchumi ambao utazingatia vilivyo shughuli za kiuchumi kwaajili ya kupunguza umasikini lakini ukijikita pia katika kuhakikisha kuwa kunakuwepo na mazingira endelevu” alielezea Bw. Mmari.

Naye Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Makamu wa Raisi Muungano na Mazingira Injinia Ngosi Mwihava alisema wao kama Serikali wametoa Baraka zote kwa kampeni hiyo kwani athari za mabadiliko ya tabia nchi zimedi kuongezeka siku hadi siku.

“Sisi kama serikali ni jukumu letu kuhakikisha wananchi wanayatunza mazingira na kuyafanya yawe endelevu, na ndio maana leo tupo hapa na vijana ili kuhakikisha elimu ya mazingira endelevu inawafikia na wao wanaisambaza” alisema Injinia Mwihava.

Aidha Injinia Mwihava alisema kuwa serikali itahakikisha mazingira yanalindwa na kuwa endelevu hivyo wataanza na kupiga marufku matumizi ya mifuko ya plastiki kuanzia Januari mwakani kama njia mojawapo wa kuzuia uchafuzi wa mazingira.

“Serikali sasa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali tunaandaa kanuni za kudhibiti mifuko ya plastiki nchini na hata kama mgeni akija nayo toka nje akifika mpakani lazima aambiwe kuwa hatutumii tena mifuko ya plastiki” alisisitiza Injinia Mwihava.

Naye mmoja wa vijana waliohudhuria hafla hiyo Pius Matunge alisema ni wakati sasa kwa vijana kushika hatamu kwenye kulinda mazingira.

"Kila kijana lazima ajione yuko mbele kwenye kulinda na kuyatetea mazingira ili yaweze kutumika kwenye kuinua uchumi wa nchi yetu" alihitimisha Bw. Pius.

Hafla hiyo iliyoandaliwa na shirika Raleigh Tanzania ilikutanisha pamoja vijana kutoka mikoa mbalimbali nchini na mashirika mbalimbali na wadau wa mazingira kujadili jinsi gani vijana wanaweza kuwa mawakala wa maendele ya Uchumi wa Kijani.

No comments: