Thursday, October 30, 2014

TIM COOK WA KAMPUNI YA APPLE ASEMA ANA FAHARI KUWA SHOGA

Mtendaji Mkuu wa Apple, Tim Cook.
MTENDAJI Mkuu wa kampuni ya Apple ya Marekani, Tim Cook, amefichua kwamba yeye ni shoga na anaona fahari kuwa hivyo.
Cook ameyasema hayo leo katika tahariri ya mtandao wa Businessweek.com kwamba: “Acha niseme wazi. Ninaona fahari kuwa shoga, na ninaona kuwa shoga ni moja ya zawadi kubwa zaidi ambazo Mungu amenipa.”
Ameongeza kusema kwamba wafanyakazi “wengi” wa Apple wanafahamu kwamba yeye ni shoga na haoni tofauti yoyote kuhusu wanavyoshirikiana naye.
Cook anakiri kwamba jambo la kufichua hali hiyo halikuwa rahisi, lakini alifanya hivyo kwa kutaka jamii imwone yuko sawa na watu wengine.
“Sijioni kuwa mwanaharakati katika jambo hili, bali ninatambua nilivyonufaika katika kujitoa mhanga kwa wengine.
Hivyo, iwapo kusikia kwamba mkuu wa Apple ni shoga kunaweza kumsaidia mtu fulani kuelewana na wengine, au kumfariji mtu yeyote anayejihisi kuwa mpweke, au kumtia moyo mtu apiganie usawa katika jamii, basi kujitoa kwangu mhanga kujifichua katika hali hii ni jambo zuri,” alisema.
Kampuni ya Apple kwa muda mrefu imepigania usawa kwa wafanyakazi wake kwa kushirikiana na Tim Cook.
Kampuni hiyo pia ilipinga wazi muswada wa bunge la Jimbo la Arizona ambao ungewaruhusu wafanyabiashara kuwabagua watu kwa misingi ya dini.
“Kampuni ambayo nina bahati kuiongoza imekuwa ikipigania haki za binadamu na usawa siku zote,” alisema Cook na kuongeza: “Tutaendelea kupigania haki zetu, na ninaamini mkuu yeyote wa kampuni hii kubwa, bila kujali rangi za watu, jinsia, au mwelekeo wa kujamiiana, atafuata msimamo huu.
Na mimi nitaendelea kupigania usawa wa watu wote hadi kieleweke.”

No comments: