Wednesday, March 03, 2010

CCJ wapata usajili wa muda



Msajili wa vyama vya siasa nchini, John Tendwa jana alihitimisha safari ya miezi miwili ya CCJ kusaka usajili wa muda,kwa kukipa chama hicho usajili wa muda.

CCJ chama ambacho kimesababisha mtikisiko ndani ya CCM kimekuwa kikifuatilia usajili wa muda katika Ofisi ya Msajili kwa karibu miezi miwili sasa tangu kuwasilisha maombi yao Januari 20, mwaka huu.

Viongozi wake wametangaza jana kwamba, wanatarajia kukamilisha kazi ya kuzunguka nchi na kupata idadi ya wanachama 200 katika kipindi cha mwezi mmoja na nusu baada ya kupata hati hiyo badala ya miezi sita.

Mwenyekiti wa CCJ Richard Kiyabo, alitumia fursa hiyo kutoa ufafanuzi wa tuhuma mbalimbali dhidi ya chama hicho na kusema hakina uhusiano wowote na Idara ya Usalama wa Taifa kwani mpango huo una lengo la kukivuruga ili kionekane ni chama pandikizi.

Kiyabo alifafanua kwamba, CCJ ni chama tofauti na vingine vya upinzani kwani kimejipanga vema kuhakikisha kinakidhi mahitaji ya msingi ya kidemokrasi kwa Watanzania.

"CCJ siyo chama cha Idara ya Usalama wa Taifa, ni chama cha usalama wa maisha ya Mtanzania, ni chama makini tofauti na vingine vya upinzani kwa hiyo kuna tofauti kubwa," alisisitiza.

Mwenyekiti huyo ambaye alikuwa akibebwa juu pamoja na katibu wake Renatus Muabhi na baadhi ya wanachama waanzilishi, alisema lengo, nia na madhumuni ya CCJ ni kushiriki uchaguzi wa Oktoba.

No comments: