Thursday, May 20, 2010

MEYA WA JIJI AKAMATWA KWA MAUAJI YA KATIBU CCM



SAKATA la kifo cha katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kata ya Isamilo wilayani Nyamagana mkoani Mwanza, Bahati Stephano (50) aliyefariki dunia baada ya kuvamiwa ofisini kwake na kuchomwa kisu, limeingia katika hatu nzito baada ya Meya wa jiji la Mwanza Leornad Bandiho Bihondo (64) (pichani) kukamatwa na jeshi la polisi kwa kuhusika.

Akizungumza na waandishi wa habari jana kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza Simon Sirro alisema kuwa kukamatwa kwa meya huyo kumetokana na taarifa za siri ambazo watuhumiwa watatu wa awali wamezitoa hivyo kufanya watuhumiwa kufikia wane.

Katibu huyo aliuawa mei 14, mwaka huu majira ya saa 6:30 mchana baada ya mtuhumiwa aliyetambulika kwa jina la Jumanne Oscar (30) kuingia ofisini kwa katibu huyo akisingizia kuwa na shida za kiofisi na baada ya kuruhusiwa kuonana naye alisikika wakibishana naye na baadaye alionekana akitoa kisu na kumchoma.

Kwa mujibu wa mashuhuda baada ya kuona mabishano hayo waliamua kufuatilia na kumuona kijana huyo akitoa kisu na kumchoma katibu huyo, upande wa titi la kushoto na tumboni, baada ya kufanya hivyo inadaiwa alitoka mbio kutaka kutokomea, lakini wasamalia wema wakiwemo wafanyakazi wenzake na marehemu wamkimbiza na kumkamata akitaka kujitosa ziwani” alisema Kamanda Sirro.

Jana akizungumza na waandishi wa habari kamanda Sirro alisema, meya Bihondo alikamatwa Juzi saa 10 alasiri katika uwanjwa wa ndege wa Mwanza alipokuwa akitokea safarini jijini Dar es salaam kwa safari zake za kikazi.

‘Bwana Bihondo tunamshikilia kama mtuhumiwa, hii ni kwa sababu baada ya kufanya mahojiano na watuhumiwa wengine watatu walimtaja yeye kuwa miongoni mwa watu ambao wanahusika. Jeshi langu bado linaendelea na uchunguzi na tutamfikisha mahakamani mara baada ya uchunguzi kukamilika” alieleza Sirro.

Bihondo anaungana na watuhumiwa wengine ambao ni Jumanne Oscar aliyekamatwa siku ya tukio na kueleza kuwa alifuatwa Kigoma kwa kazi ya kuua na mtuhumiwa Baltazal Shushi (43) ambaye naye baada ya kutiwa mbaroni alimtaja kampeni meneja wake Abdul Hausi (45) wote wamekamatwa.

Alisema licha ya Bihondo kukamatwa bado kuna watuhumiwa wengine wanatafutwa na jeshi lake (lakini hakuwataja kwa sababu za kuhofia kuharibu upelelezi) na kusisitiza kuwa jeshi lake litahakikisha linawatia mbaroni na kukomesha mtandao wa watu waliozoea kuhusika na mauaji.

‘Niwaombe wananchi wazidi kutoa ushirikiano, kwani bila ya ushirikiano jeshi langu halitaweza kuwabaini mtandaao wa wauaji” alisisitiza Sirro. Habari hii imeandikwa na Frederick Katulanda. SOURCE: MWANANCHI

No comments: