Sunday, May 23, 2010

Twiga Stars yaiangamiza Eritrea 8-1



TIMU ya taifa ya Tanzania ya wanawake Twiga Stars imetoa kipigo cha mbwa mwizi kwa Eritrea kwa kuichakaza kwa mabao 8-1 kwenye mchezo wa kutafuta tiketi ya kufuzu kwa fainali za mataifa ya Afrika.

Mshambuliaji wa Twiga Stars, Mwanahamisi Omary alifunga mabao manne peke yake huku Asha Rashidi akiziona nyavu hizo mara tatu kwenye karamu hiyo kubwa ya mabao iliyoshudiwa ikitokea kwenye uwanja wa Uhuru.

Twiga ilipata bao lake la kwanza dakika ya sita lilofungwa na nyota wa mchezo huo Mwanahamisi aliyeunganisha vizuri mpira wa adhabu uliopigwa na Ester Chaburuma.

Kuingia kwa bao ilo kuliamsha ari ya Twiga Stars ilipata bao la pili dakika ya 19, limefungwa na nahodha Sophia Mwasikili kwa shuti la umbali wa mita 18, akipokea pasi mzuri kutoka kwa Etoe Mlezi.

Wakati Eritrea wakijuliza nini kinatokea Asha Rashidi aliwalamba chenga mabeki na kupiga shuti lililomshinda kipa Semhar Bekit na kujaa wavuni kuwa bao la tatu.

Mwanahamisi alifunga bao la nne dakika 27 kwa ufundi kwa kumchenga kipa Bekit alikipokea pasi ya Fatuma Khatib kufanya matokeo kuwa 4-0 hadi mapumziko.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na wenyeji walipata bao la tano dakika 60 kupitia kwa Asha kabla ya Mwanahamisi kufunga la sita dakika 62.

Mchezo huo uliokuwa wa upande moja kwani Eritrea walionekana kushindwa kuendana na kasi ya mchezo walijikuta wakifungwa bao la saba na nane yaliyofungwa na Rashidi (74) akipokea pasi ya Etoe naye Mwanahamisi
alifunga bao lake la nne dakika 78, akimalizia kazi ya Rashidi.

Eritrea ilipata bao la kufutia machozi kupitia kwa Rahwa Solomon aliyewapiga chenga mabeki na kufunga bao hilo dakika ya 90.

Makocha wa Twiga Stars, waliokuwa mafunzoni nchini Brazil, Charles Boniface Mkwasa na Adold Richard wamewasiri uwanjani hapa na kukaa kwenye viti maalumu.

Naye waziri Geogre Mkuchika amewapongeza Twiga Stars kwa ushindi mkubwa walioupata na kuwataka waongeze juhudi ili wafanye vizuri kwenye mechi ya marudiano.

Huku akiahidi kushirikiana na TFF katika kutafuta mkoa wenye baridi kwa ajili ya kuweka kambi ya timu hiyo. Imeandikwa na Doris Maliyaga; SOURCE:MWANANCHI

No comments: