Thursday, March 26, 2009

Mzee malechela awaka




Mwanasiasa mkongwe, John Malecela, ametaka malumbano ya kisiasa yanayoendelea sasa kwa wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) yakome mara moja na hayana msingi katika maendeleo ya nchi.

Malecela (75), ambaye ni Mbunge wa Mtera (CCM) pia aliwahi kuwa Waziri Mkuu, Makamu wa Rais na Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, aliyasema hayo Dar es Salaam jana.

Akizungumza na waandishi wa habari nyumbani kwake Sea View, Malecela alisema si vyema wala busara kuendesha malumbano kupitia vyombo vya habari ilhali kuna mamlaka zinazohusika.

“Kama mwanasiasa wa kawaida na Mtanzania, ningependa kusema kuwa malumbano haya katika vyombo vya habari, ningeomba yakome, maana hayawasaidii Watanzania,” alisema Malecela.

Aliwataka wahusika katika malumbano hayo ambayo hata hivyo hakuwataja kwa majina, watumie vyombo husika kuwasilisha hoja zao.

Alisema ni vyema kila jambo likapelekwa katika chombo husika, ambavyo ni vyama, Bunge na serikali ambako yatashughulikiwa ipasavyo na si kuwachanganya wananchi.

Malecela alisema malumbano haya huchangiwa na vyeo, fedha na mambo mbalimbali waliyonayo wanaolumbana.

Aidha, alivitaka vyombo vya habari nchini kuendelea kuelimisha jamii na kufichua maovu na si kujiingiza katika malumbano na kushabikia malumbano hayo yasiyo jenga.

“Vyombo vya habari vifanye kazi zake na visikubali kutumiwa na watu wachache na kuwaharibia hadhi yenu kitaaluma, na itafika mahali watu watadhani kuwa nia ya vyombo vya habari ni kutukanana na kuendesha mijadala isiyo na manufaa,” aliongeza.

Pia alimtaka waziri mwenye dhamana na Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo, George Mkuchika, achuje utitiri wa magazeti yaliyopo kwa sasa nchini ambao ni wa juu kuliko nchi yoyote barani Afrika.

Akizungumzia hoja za kumeguka kwa CCM, Malecela alisema hiyo ni ndoto na wanaotumia nukuu ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ya kuwa “Mimi nang’atuka lakini ninaendelea kuamini bila CCM madhubuti nchi itayumba,” kuwa si sahihi.

Alisema iwapo kuna mwana CCM anataka kumeguka, afanye hivyo na hawatayumba kamwe na kufafanua kwa Kiingereza “we won’t miss them (hatutawajutia)” wanaotaka wajimege sasa, CCM bado ina nguvu.

Akitoa mfano wa watu waliojimega tangu kuundwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, alisema viongozi wa upinzani wote wametoka CCM lakini hakuna kilichoiharibu CCM isipokuwa imezidi kusonga mbele.

No comments: