Wednesday, March 04, 2009

ICC yaidhinisha al-Bashir akamatwe


THE HAGUE, Uholanzi

MAHAKAMA Kimataifa ya Uhalifu wa kivita (ICC) imetoa hati ya kutaka kiongozi wa Sudan, Omar al-Bashiri (65) kukamatwa, kutokana na kuhusishwa na uhalifu katika mazingira ya vita, ikiwa ni hati ya kwanza kutolewa kwa ajili ya mkuu wa nchi aliye madarakani.

Jopo la majaji watatu wa mahakama hiyo lilieleza jana kuwa uamuzi huo wa kutaka al-Bashir akamatwe unatokana na kuwepo kwa ushahidi wa kutosha kuhusiana na mauaji yaliyotokea katika eneo la Darfur.

“Leo, chemba ya uchunguzi wa awali ya mahakama hii ya ICC inatangaza kutolewa kwa hati ya kukamatwa kwa rais wa Sudan kwa tuhuma za uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya ubinadamu,” msemaji wa ICC, Laurence Blairon alieleza jana.

“Anatuhumiwa kwa kuwajibika katika uhalifu, kwa kutumia mamlaka yake kuagiza kufanyika kwa mashambulizi dhidi ya maeneo muhimu ya raia huko Darfur Sudan, mauaji, utesaji, ubakaji, udhalilishaji na kuhamisha idadi kuba ya raia kwa nguvu, pia kuchukua mali zao.

Katika mkutano maalum wa vyombo vya habari, Blairon alisema kuwa Bashir na viongozi wengine wa juu wa kisiasa na wa kijeshi wa Sudan wanawajibika kwa kuchochea na kupanga mashambulizi yaliyosababisha mateso makali na vifo kwa watu waishio eneo hilo la Darfur.

Japokuwa hakukuwa na jibu wala mwitikio wa aina yoyote kutoka Sudan muda mfupi baada ya kutangazwa kwa uamuzi huo wa ICC dhidi ya Bashir, juzi rais huyo wa Sudan alipuuza suala la kutolewa kwa hati hiyo akisema halina maana.

No comments: