Sunday, March 15, 2009

Mzee Shaaban Mloo afariki dunia



The Civic United Front (CUF – Chama cha Wananchi) kinasikitika kuwaarifuni kwamba, leo asubuhi mwasisi wa chama hiki, Shaaban Khamis Mloo, amefariki dunia, nyumbani kwake, mjini Zanzibar. Mazishi yake yalifanyika jana saa 10.00 alasiri huko huko Zanzibar.

Marehemu Mzee Mloo alikuwa katibu mkuu wa kwanza wa CUF kwa miaka nane, kutoka 1992 hadi 2000 alipochukua nafasi ya umakamo mwenyekiti hadi alistaafu mwaka 2004. Yeye ndiye miongoni mwa waasisi wa Chama hiki, kwa kuanzia na vuguvugu la KAMAHURU. Ni yeye ndiye aliyeongoza mazungumzo ya kwanza na aliyekuwa mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CCW), James Mapalala, na hatimaye kuungana na kuzaliwa kwa CUF tuliyonayo sasa.

Kwa hivyo, CUF inamtambua Mzee Mloo sio tu kama kiongozi mstaafu wa Chama, bali zaidi kama mwasisi, mwanzilishi na mwanachama imara na shupavu katika siku zote za uhai wake. Atakumbukwa daima ndani na nje ya CUF kama mjuzi wa siasa za Zanzibar na za Tanzania kwa ujumla, mchapakazi na mtu aliyekuwa na ujasiri wa kupigiwa mfano.

Hata baada ya kustaafu umakamo mwenyekiti, Mzee Mloo aliendelea kuwa sehemu muhimu ya CUF kwa kujitolea katika mashauri mbali mbali. Kila alipokuwa na uwezo, hakuacha kuhudhuria mikutano ya hadhara au vikao vyovyote ambavyo alialikwa.

Kikao cha mwisho kuhudhuria ni Mkutano Mkuu wa Nne wa chama chetu uliofanyika katika ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam, kuanzia 23 hadi 27 Februari, mwaka huu. Kwa hivyo, hadi siku za mwisho mwisho wa uhai wake, Mzee Mloo alisimama imara kuijenga na kuihuisha CUF.

1 comment:

Anonymous said...

innalilahi wainnailahim rajiuun.M,Mungu amlaze mahali pema peponi amin.