Tuesday, January 22, 2008

Meghji: Wanannchi hawana imani na BoT

* Asema ni kutokana na ufisadi uliobainika
* Asema itachukua muda mrefu kuisafisha
* Aagiza Bodi mpya kurejesha hadhi yake
* Asifu mafanikio kiduchu yaliyopatikana



Na Muhibu Said wa Mwananchi

SERIKALI imesema ufisadi wa mabilioni ya shilingi uliobainika katika Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ndani ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), umepoteza imani ya wananchi kama chombo thabiti na makini katika utekelezaji wa majukumu yake.

Kauli hiyo ambayo ni ya kwanza kutolewa na serikali tangu ufisadi huo ubainishwe na kampuni ya nje ya ukaguzi ya Ernst & Young, ilitolewa na Waziri wa Fedha, Zakhia Meghji alipokuwa akizindua bodi mpya ya BoT, jijini Dar es Salaam jana.

Alisema bodi hiyo ambayo inaongozwa na Gavana mpya wa BoT, Profesa Benno Ndulu, inaanza kazi katika mazingira ambayo wananchi wamepoteza imani juu ya BoT kama chombo thabiti na makini katika utekelezaji wa majukumu yake kutokana na matukio ya hivi karibuni yanayohusiana na upotevu wa fedha nyingi za umma chini ya EPA.

"Matukio haya yametia doa kubwa katika sifa za taasisi hii muhimu na itachukua muda na juhudi kubwa kurudisha imani ya wananchi kwa chombo hiki," alisema Waziri Meghji.

Kutokana na hali hiyo, Waziri Meghji aliitaka bodi kuhakikisha inachukua hatua madhubuti kurejesha imani miongoni mwa wananchi kutokana na taarifa za kuhusika kwa BoT katika malipo haramu au ambayo uhalali wake unatia shaka, ikiwa ni moja ya mikakati ya bodi hiyo ya kukabiliana na changamoto kubwa zinazoikabili.

No comments: