Friday, January 11, 2008

CUF wakunwa na Kikwete

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Kufuatia taarifa ya Ikulu iliyoelezea maamuzi na hatua
zilizoagizwa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete kuhusiana
na ukaguzi wa nje wa Benki Kuu ya Tanzania, Katibu
Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, ametoa taarifa
ifuatayo:

“Chama Cha Wananchi (CUF) kimepokea na kutiwa moyo na
maamuzi na hatua zilizoagizwa na Rais Jakaya Mrisho
Kikwete za kukabiliana na ufisadi uliopindukia mipaka
katika Benki Kuu ya Tanzania. Hatua hii imeleta
matumaini kwa wananchi walio wengi kwa kuona kuwa Rais
na Serikali ya Jamhuri ya Muungano imeanza kuchukua
hatua madhubuti dhidi ya watumishi wa Serikali
wanaojihusisha na hujuma kwa mali ya Watanzania.

Natoa pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Rais Jakaya
Kikwete kwa maamuzi mazito aliyoyachukua katika
kipindi hiki ambacho wananchi walikuwa na shauku kubwa
kuona ni kwa uzito gain Rais angelilichukulia tatizo
hili linaloelekea kuota mizizi nchini.

CUF inatoa wito kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini,
Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU na Mwansheria Mkuu wa
Serikali kukamilisha, katika kipindi kifupi
iwezekanavyo, kazi waliyotumwa na Rais ya kutumia
madaraka waliyokabidhiwa kufanya uchunguzi wa kina, na
kisha kuwachukulia hatua za kisheria wahujumu wote wa
uchumi wa taifa letu bila ya woga, chuki wala
upendeleo.

Aidha CUF inatoa wito kwa Rais kuendeleza kwa makini
mapambano ya dhati dhidi ya wote waliojihusisha,
wanaojihusisha nawatakaojihusisha na vitendo vya aina
mbali za hujuma dhidi ya rasilimali za nchi yetu na
fedha za umma bila ya kujali vyeo vyao, umaarufu wao
na utukufu wao. Namhakikishia Rais kuwa mimi na CUF
tutaendelea kumuunga mkono katika juhudi zake za
kuokoa mali ya taifa letu na kusimamia maadili ya
uongozi na utumishi wa umma.

CUF pia inatoa pongezi maalum kwa Kambi ya Upinzani
Bungeni chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Hamad
Rashid Mohamed kwa ujasiri wao wa kuisaidia Serikali
katika kufichua maovu yanayotendwa na wale
waliokabidhiwa majukumu ya kuwatumikia Watanzania
lakini badala yake wakajinufaisha binafsi bila ya
kuwaonea huruma raia masikini wa nchi hii. Ni
matumaini yangu kuwa Serikali itaendelea kushirikiana
na Kambi ya Upinzani katika kujenga enzi mpya ya siasa
za kistaarabu na za mashirikiano zinazovuka mipaka ya
itikadi kwa mambo yanayohusu maslahi ya taifa letu.

CUF inatoa wito kwa wananchi wote kuwa macho katika
kulinda rasilimali za nchi yetu na kutoa taarifa kwa
mamlaka zinazohusika, wakiwemo wabunge, kwa zile
hujuma ambazo wana ushahidi nazo.

CUF siku zote itashirikiana na Serikali, Bunge, na
watu wote wenye uzalendo na nia ya dhati ya kuisafisha
nchi yetu na uoza ambao kama utaachiwa uendelee
utaliangamiza taifa letu.”

DAR ES SALAAM
11 Januari, 2007


Directorate of Information and Policy Dissemination
The Civic United Front (CUF)
Party Headquarters
P.O. Box 3637
Zanzibar
Tanzania
Tel. (+)255 (0)747 414100 / (+)255 (0)741 257 665
E-mail: cufhabari@yahoo.com
Website: www.cuftz.org

No comments: