Wednesday, August 16, 2017

Wananchi watakiwa kujiunga na Mfuko wa Afya

 Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese akizungumza wakati wa kampeni ya afya aliyoizindua kijiji cha Malwilo kata ya Somagedi.
 Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kishapu, Dk. Josephat Shani ambaye pia mganga mkuu wa wilaya akizunguza wakati wa uzinduzi huo.
 Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Maguja Daniel akitoa neno wakati wa uzinduzi huo. 
 Mratibu wa Mradi wa Tuimarishe Afya (HPSS) mkoa wa Shinyanga, Haruni Kasale akizungumzia umuhimu kwa wananchi kujiuna na mfuko wa CHF iliyoboreshwa.
 Sehemu ya wananchi wa kijiji cha Malwilo wakifuatilia uzinduzi wa kampeni ya afya.
 Ofisa Teknolojia, Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wilaya ya Kishapu, Jacob akitoa ufafanuzi kuhusu mradi huo wa CHF.
 Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese akizungumza na wananchi katika kijiji cha Malwilo wakati wa uzinduzi wa kamnpeni hiyo ya afya.
Wananchi wakifuatilia matukio hayo.

Na Robert Hokororo, Kishapu DC.

Wananchi wametakiwa kujiunga na Mfuko wa Afya (CHF) iliyoboreshwa ili wapate huduma na kuboresha afya zao na hivyo kuweza kushiriki shughuli mbalimbali za uzalishaji.

Wito huo ulitolewa jana na Katibu Tawala Wilaya ya Kishapu, Shadrack Kangese wakati akizindua kampeni ya uhamasishaji shughuli za afya wilayani hapa.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa wilaya hiyo katika kijiji cha Malwilo, Mheshimiwa Nyabaganga Taraba, Kangese aliwataka viongozi wa serikali za vijiji kuonesha mfano kwa kujiunga na mfuko huo mapema.Kangese pia aliwataka viongozi hao kuhamasisha kaya zingine zijiunge ifikapo Oktoba mwaka huu wakiwemo walengwa wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF). 

Alisema huduma hiyo ni muhimu kwa wananchi wasiojiweza na wenye kipato cha chini ambapo kwa sh. 10,000 humuwezesha kuhudumiwa yeye na watu wengine sita katika kaya kwa mwaka mzima.

Alisema Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya kwa kutengeneza miundombinu, kutoa vifaa tiba na kuongeza wataalamu wa sekta hiyo ili waweze kuhudumia wananchi kwa ufanisi.Katibu Tawala huyo aliongeza kuwa utekelezaji wa mradi wa CHF iliyoboreshwa ulianza rasmi Machi 2016 kwa kuimarisha mfumo wa fedha na uoreshaji dawa na vifaa tiba.

Aidha, alisema katika wilaya hiyo ni kaya 10,756 zimeandikishwa huku lengo likiwa ni kaya 42,000 ambapo kila mwananchama anapata kadi na matibabu mwaka mzima.Aliwataka watumishi wa afya pamoja na changamoto ya uchache waendelee kuhudumia wananchi kwa kufuata sheria, taratibu na miongozo iliyopo wakati Serikali inaendelea na michakato ya kuongeza wengine.

Kwa upande wake, mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kishapu, Dk. Josephat Shani aliwataka wajawazito kuhudhuria kliniki ili kujifungua salama.Alisisitiza umuhimu kwa wanawake kujifungulia katika hosptali ili kupata huduma stahiki pamoja na mtoto na kuwa katika hali ya usalama tofaui na nyumbani.

Dk. Shani ambaye pia ni mganga mkuu wa wilaya pia aliwataka kufuata maelekezo ya watoa huduma za afya ili kuepuka kupata matatizo yanayoweza kutokea wakati wa kujifungua. 

No comments: