Saturday, August 19, 2017

Serikali Yathibitisha Ujio wa Bombadier Mpya uko palepale

ZAWA1
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari – MAELEZO, Bibi. Zamaradi Kawawa akisisitiza jambo wakati wa mkutano wake na Waandishi wa Habari leo Jijini Dar es Salaam kuhusiana na taarifa za kuzuiwa kwa ndege ya Serikali aina ya Bombadier ambayo inatengenezwa nchini Canada.  (Picha na: Idara ya Habari – MAELEZO)
ZAWA2
Na Mwandishi Wetu-MAELEZO
Serikali imethibitisha na kuwahakikishia Watanzania kuwa ujio wa ndege mpya ya tatu aina ya Bombardier Q400-Dash 8 upo pale pale licha ya baadhi ya wanasiasa wasio wazalendo kutumia kila njia kukwamisha ujio huo.
Kauli ya kuthibitisha ujio wa ndege hiyo imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Habari (MAELEZO) na Msemaji Mkuu wa Serikali Bi. Zamaradi Kawawa wakati akiongea na Waandishi wa Habari leo Jijini Dar es Salaam.
Alieleza kuwa kuchelewa kwa ndege hiyo ambayo ilitakiwa kuwasili mwezi Julai mwaka huu kumetokana na majadiliano yanayoendelea ambayo kimsingi yamechangiwa na baadhi ya wanasiasa wasio wazalendo kushiriki kwao moja kwa moja kuweka zuio mpaka pale majadiliano yatakapo kamilika.
 “Kuna baadhi ya Watanzania wenzetu wenye maslahi binafsi wanapiga vita ndege hii kuletwa nchini lakini Serikali inawahakikishia wananchi kuwa ndege itakuja na hakuna sababu ya kuwa na wasiwasi”, alisisitiza Zamaradi.
Alieleza kuwa Serikali iliishapata fununu kuwa kuna kuna baadhi ya viongozi wa chama cha siasa wana mpango wa kukwamisha juhudi za ujio wa ndege mpya na kwamba bila hata chembe ya uzalendo, watu hao wamejidhihilisha wenyewe hadharani kwamba wapo nyuma ya pazia la kuhujumu jitihada za Serikali kwa maslahi yao binafsi.
“Serikali imesikitishwa sana kwa hujuma zinazofanywa waziwazi na kwa ushabiki wa hali ya juu na baadhi ya viongozi wa kisiasa kupingana na mwelekeo mzuri wa Rais wa kuleta maendeleo”, alieleza Zamaradi.
Aidha alisema kuwa Serikali imeanza kuchukua hatua za diplomasia na za kisheria kwa wote wanaoshabikia na kutengeneza migogoro na hujuma mbalimbali dhidi ya maendeleo ya nchi yetu.
Kwa mujibu wa Zamaradi, kuna wanasiasa waliokwenda kufungua madai kwamba Serikali ya Tanzania inadaiwa na kwamba ndege hiyo ishikiliwe hawana uhalali wowote wa kufanya hivyo na ni vibaraka waliotumwa na wapiga dili wasioitakia mema Tanzania.
Katika siku za hivi karibuni kumeibuka baadhi ya wanasiasa Watanzania ambao wamekuwa wakitoa kauli zenye lengo la kuhujumu maendeleo ya nchi ikiwemo kushawishi wafadhili kuinyima misaada Tanzania lakini pamoja na jitihada hizo, washirika wa maendeleo wameendelea kuongeza misaada kwa Tanzania kutokana na kuridhishwa na hatua mbalimbali za Serikali katika kupambana na rushwa na ufisadi na kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo.

No comments: