Wednesday, September 25, 2013

TIKETI KENYA AIRWAYS SASA KWA M PESA

Mkuu wa Idara ya Uendelezaji Teknolojia ya Habari wa Shirika la Ndege la Kenya Henry Obare (kushoto) na Mkuu wa Idara ya Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania Kelvin Twissa wakimfuatilia Ahmed Abdallah Said jinsi anavyolipia tiketi yake ya ndege kwa njia ya M-pesa kutoka katika simu yake ya kiganjani. Said amekuwa mteja wa kwanza kutumia huduma hiyo muda mfupi baada ya kuzinduliwa leo jijini Dar es Salaam. 
Mkuu wa Idara ya Uendelezaji Teknolojia ya Habari wa Shirika la Ndege la Kenya Henry Obare (kushoto) akimkabidhi mteja Ahmed AbdallaH Said tiketi yake ya safari ya nje ya nchi baada ya kuilipia kwa njia ya M-pesa muda mfupi baada ya huduma hiyo kuzinduliwa jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Kelvin Tiwissa. Huduma hiyo itawawezesha wasafiri wa  Shirika la Ndege la Kenya kulipia tiketi zao kwa M-pesa na hivyo kuwapunguzia gharama za safari na usumbufu wa foleni.

Waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini wakifuatilia uzinduzi wa ubia wa kibiashara kati ya M-pesa na Shirika la Ndege la Kenya ambapo kuanzia sasa wasafiri wa shirika hilo wanauwezo wa kulipia tiketi zao za safari zote za shirika hilo wakati wote mahali popote kwa njia ya M-pesa. 

Meneja Uendelezaji huduma ya M-pesa Francis Tewele akimuelekeza mteja wa Shirika la Ndege la Kenya Ahmed Abdallah Said jinsi ya kulipia tiketi ya Shirika hilo la Ndege kwa njia ya M-pesa wakati wa hafla ya uzinduzi wa huduma hiyo jijini Dar es Salaam. Wanaoshuhudia  kutoka kushoto ni Mkuu wa Uendelezaji Teknolojia ya Habari wa Shirika la Ndege la Kenya Henry Obare, Meneja Uhusiano wa Nje wa Vodacom Salum Mwalim na Mkuu wa Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Kelvin Twissa.

Dar es Salaam 24 Septemba 2013 Shirika la Ndege la Kenya – Kenya Airways limeingia ubia na kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom kupitia huduma yake ya M-pesa kuwawezesha wateja wake kulipia tiketi zao ikiwa ni kwa mala ya kwanza kwa huduma hiyo kuingia ubia na Shirika la la Ndege la Kimataifa kuwawezesha wateja wake kufanya malipo kwa njia ya simu za mkononi.
Akizungumza Wakati wa kutangaza rasmi ubia huo jijini Dar es salaam leo Mkuu wa Kitengo cha Masoko na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Kelvin Twissa, amesema ni furaha kubwa kuona M-pesa ikiendelea kupanuka katika ngazi ya kimataifa ikiwa ni moja ya mafanikio makubwa kwa huduma hiyo kuendelea kurahisisha maisha ya Watanzania.
“Leo tunaandika historia tukiendeleza ahadi yetu kwa watanzania kupitia M-pesa kuwa tutaendelea kutoa suluhusho la njia rahisi na ya uhakika katika kufanya malipo, utumaji na upoekaji wa fedha mahali popote Wakati wowote.”Alisema Twissa.
“Kupitia mtadao wetu mpana ni wazi kwamba sasa tumeyarahisha zaidi maisha ya maelfu ya watanzania wanaotumia huduma za Shirika la Ndege la Kenya kwa shughuli za kiuchumi na kijamii kuwa na njia rahisi zaidi ya kulipia tiketi za safari zao bila kuingia gharama za kulazimika kufika vituo vya mauzo ya tiketi na kupanga foleni.”Aliongeza
Twissa amesema M-pesa itaendelea kutoa suluhisho la mahitaji ya watanzania na soko kwa ujumla kwa kuziunganisha biashara mbalimbali na wateja na kwamba hilo halitobadilika.
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Kitengo cha Taarifa Ukuzaji Teknolojia wa Shirika la Ndege la Kenya, Henry Obare, ameelezea matumaini yake kwa shirika hilo kutumia teknolojia za kisasa zaidi katika kukuza biashara kwa kuhakikisha linawahudumia wateja wake kwa haraka na usalama zaidi.
“Katika nchi yenye shughuli nyingi za kitalii na biashara huku shirika letu likiwa mstari wa mbele katika kufanikisha shughuli hizo kwa kuwezesha watu wake kuingia na kutoka ndani ya nchi kwa uhakika tunayo kila sababu kumuwezesha kila mmoja na njia kuwa na fursa ya kunufaika na uwepo wetu.”Alisema Obare na kuongeza.
“Tunaamini ya kwamba hii ni siku kubwa sana katika historia ya shirika letu tunapokamilisha ndoto yetu ya kuwapatia kile ambacho wamekuwa wakikisubiri kutoka kwetu kwa muda mrefu.”  Alihitimisha Obare.
Ili kulipia tiketi kwa M-pesa mteja anapaswa kupiga *150*00# na kuchagua kipengele na biashara na kufuata maelekezo.
Hata hivyo mteja atatakiwa kwanza kuwa na nambari ya kumbukumbu ya tiketi yake pamoja na gharama za tiketi husika kutoka Ofisi za Shirika hilo ambazo ataziingiza wakati akifanya muamala wa malipo.
Ushirikiano na Shirika la Ndege la Kenya ni wa pili kwa M-pesa kuvuka mipaka ya Tanzania ukitanguliwa na ushirikiano kati yake na Western Union unaomuwezesha mteja wa M-pesa kuwa na uwezo wa kupokea fedha kutoka nchi yoyote duniani ambayo Western Union inafanya kazi.

No comments: