Wednesday, September 25, 2013

Jakaya Kikwete atuma salamu za Rambirambi kwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bibi Fatma Mwassa kufuatia kifo cha Mkuu wa Wilaya ya Urambo Bibi Anna Magoa


THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
 DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
 Rais Jakaya Mrisho Kikwete ametuma salamu za Rambirambi kwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora Bibi Fatma Mwassa kufuatia kifo cha Mkuu wa Wilaya ya Urambo Bibi Anna Magoa kilichotokea tarehe 24 Septemba, 2013 katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar-Es-Salaam.

Katika salamu hizo, Rais amemuelezea Bibi  Magoa kuwa alikuwa kada na mchapakazi hodari ambaye ameacha pengo kubwa katika Chama na Serikali.

“Kwa hakika umepoteza moja ya nguzo zako mkoani Tabora. Bibi Anna amekua kada na mtumishi wa kutumainiwa katika Chama chetu cha Mapinduzi na serikali kwa ujumla. Tumeondokewa na mtu muhimu na mchapa kazi hodari” Rais amesema na kumuomba Bibi Fatma Mwassa kumfikishia salamu za pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa na marafiki zake wote.

Rais pia amewatumia salamu za pole wafanyakazi na wananchi wa Urambo ambao marehemu amekuwa akifanya nao kazi tangu alipohamia Wilayani humo  Mwaka 2010.

Marehemu ameacha mtoto mmoja wa kike na wajukuu wawili. Mwili wake unatarajiwa kusafirishwa leo kwenda Mkoani Iringa kwa maziko.

Imetolewa na:

Premi Kibanga,
Mwandishi wa Habari wa Rais, Msaidizi,
Ikulu
Dar-Es-Salaam, Tanzania
25 Septemba, 2013

No comments: