Tuesday, August 23, 2011

Mwanawe Gaddafi aapa kupambana na waasi

Mwanawe Gaddafi Saif al-Islam

Mtoto wa kiume wa Kanali Muammar Gaddafi, Saif al-Islam, ambaye awali waasi walidai kuwa wamemkamata, amejitokeza katika hoteli moja inayoshikiliwa na wafuasi wa Kanali Gaddafi.

Mwandishi wa BBC Matthew Price amezungumza na Saif al-islam na kusema kuwa anaonekana kuwa mchangamfu na shauku kuu.

Saif al-Islam amesema waasi wameingia kwenye ''mtego'' mjini Tripoli na kwamba wanajeshi wanaomuunga mkoni Kanali Gaddafi walikuwa ''wamevunja uti wa mgogo wa waasi hao''.

Waasi wanaopigana kuudhibiti mji mkuu wa LibyaTripoli , wamerudishwa nyuma na wanajeshi wanaomuunga mkono Kanali Muammar Gaddafi.

Lakini wakati mapigano yanapoendelea katika maeneo mbalimbali ya mji, msafara wa waasi kutoka mashariki mwa nchi ulirudishwa nyuma.

Bado hajulikani alipo Kanali Gaddafi

Jumapili iliyopita waasi walidai kuwa walikuwa wamemkamata Saif al-Islam, pamoja na familia yake.

Hata hivyo, bado Kanali Gaddafi hajulikani alipo. Nyumba yake inalindwa na wapiganaji wanaomtii.

Waasi hao walioingia mjini Tripoli jumamosi iliyopita walikaribishwa watu waliokuwa wakisheherekea katika bustani ya Green Square wakati walipowasili siku ya jumapili.

Waasi hao wamesema kuwa wameweka vizuizi katika sehemu mbalimbali za mji lakini wanakabiliwa na upinzani mkali katika baadhi ya maeneo.

Kamanda wa waasi amesema wanadhibiti asilimia 90 ya mji wa Tripoli.

Kiongozi wa Baraza la Mpito la kitaifa (NTC), Mustafa Abdel Jalil, amesema wakati wa ushindi halisi utakuwa pale watakapo mkamata Kanali Gaddafi.

Rais Obama apongeza watu wa Libya

Rais Barrack Obama amewapongeza watu wa Libya kwa kile alichokitaja kama ''kujitolea mhanga kusipokuwa kwa kawaida''. Obama amesema watu wa Libya wanakaribia kupata kile wanachohitaji.

Katibu mkuu wa Umoja wa mataifa, Ban Ki-Moon naye amewakumbusha wanachama wa Umoja huo kuwa, wanajukumu la kuheshimu mahakama ya kimataifa ya jinai, ambayo imetoa hati za kuwakamata Kanali Gaddafi, mtoto wake wa kiume Saif al Islam na mkuu wake wa idara ya ujasusi.

Baadhi ya viongozi wa waasi wanasema afadhali wafunguliwe mashtaka nchini Libya na sio katika mahakama ya kimataifa ya ICC, mjini The Hague.

No comments: