Monday, June 08, 2009

Tanzania yamwagiwa mabilioni ya bajeti


WASHIRIKA WA MAENDELEO KUTOA MISAADA YA BAJETI KWA TANZANIA YA SHILINGI BILIONI 901 KWA MWAKA WA FEDHA 2009/10

Washirika wa Maendeleo wanaotoa misaada ya bajeti kwa Tanzania wameendelea na dhamira yao ya kuchangia bajeti ya Serikali. Kwa mwaka wa fedha wa 2009/10 wanatarajia kutoa shilingi za Kitanzania bilioni 901 kupitia mfuko mkuu wa Serikali. Hiki ni kiasi kikubwa cha fedha kwa bajeti ya Serikali na kinatarajiwa kugharamikia shughuli muhimu za maendeleo katika nchi.

Uamuzi wa kutoa kiasi hiki cha fedha unatokana na majadiliano muhimu na yenye kujenga kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo kupitia kalenda ya mwaka ya majadiliano ya misaada ya bajeti. Majadiliano haya ambayo hulenga katika masuala muhimu ya kupunguza umaskini kwa Tanzania ni muhimu sana katika uamuzi wa utoaji misaada ya jinsi hii.

Kwa mujibu wa Dk. Sipho S. Moyo, Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika hapa Tanzania na Mwenyekiti wa kundi la Wahisani wanaotoa misaada kupitia Mfuko Mkuu wa Serikali:

“Tunashukuru kwa kuwa Mwenyekiti wa Washirika wa Maendeleo wanaotoa Misaada ya Bajeti. Ni muhimu kuanza jukumu hili nyeti kama Mwenyekiti kwa kutoa taarifa ya misaada ya bajeti itakayotolewa kwa Tanzania. Misaada hii ya bajeti inaonesha dhamira ya dhati ya kuendelea kushirikiana na kufanya kazi pamoja na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kutafuta njia endelevu ya kuleta maendeleo, kupunguza umaskini na ustawi wa Taifa”.

Kufuatia matokeo ya mapitio ya mwaka ya misaada ya bajeti, Washirika wa Maendeleo wameweza kuthibitisha mchango wao wa misaada ya bajeti kwa mwaka 2009/10. Kiasi hiki cha misaada kinaendana na hatua ya maendeleo ambayo serikali imekuwa ikifanya, japo changamoto bado zipo zinazohitaji kutatuliwa pamoja na makubaliano yaliyofikiwa katika mapitio ya mwaka.
Washirika wa Maendeleo wanaotoa misaada ya bajeti ni pamoja na: Benki ya Maendeleo ya Afrika, Canada, Denmark, Jumuiya ya Ulaya,Finland, Ujerumani, Ireland, Japani, Uholanzi, Norway, Sweden, Switzerland, Uingereza, na Benki ya Dunia.
Kwa taarifa zaidi wasiliana na : Ofisi ya Benki ya Maendeleo ya AfriKa hapa Tanzania: Simu Namba + 255 22 212 5281-2

No comments: