Friday, June 19, 2009

Rubani afa ndege ikiwa angani

Katika kisa ambacho wengi watadhani ni muujiza, abiria 247 waliokuwa wakisafiri na ndege ya kampuni ya Continental kutoka Ubelgiji hadi Marekani waliponea chupuchupu wakati nahodha wa ndege yao alipofariki dunia.
Msemaji wa Halmashauri inayosimamia usafiri wa ndege Marekani, Arlene Salac alisema kulikuwa na marubani wengine wawili ambao waliidhibiti ndege hiyo aina ya Boeing 777 hadi uwanja wa ndege wa Newark Liberty ambako ilitua kwa dharura.
Mtaalamu mmoja wa usafiri wa ndege, Jim Ferguson alisema si jambo la kawaida rubani kufariki dunia akiwa angani.
Kwa kawaida ndege hiyo huendeshwa na marubani wawili. Lakini kwa bahati nzuri wakati huu, kulikuwa na mwingine wa ziada.
Bwana Ferguson alisema ingekuwa vigumu kwa rubani mmoja kuidhibiti ndege hiyo kutua.
Abiria hawakuambiwa lolote kuhusu mkasa huo. Miongoni mwao alikuwa daktari mmoja wa maswala ya moyo, Dr. Julien Struyven ambaye aliitikia tangazo daktari yeyote kwenye ndege hiyo kujitokeza.
Abiria hawakujua kwamba mwito ulitolewa kwa ajili ya kumuokoa rubani wa ndege hiyo.
Dr Struyven alipomfikia rubani huyo alikuta kama tayari ameaga dunia.
“Hakukuwa na uwezekano wowote wa kumwokoa,” alisema Dr Struyven.
Alisema huenda rubani huyo mwenye umri wa miaka 60 na ambaye amehudumia kampuni hiyo kwa zaidi ya miaka 20 alifariki dunia kutokana na matatizo ya moyo. Kwa habari zaidi soma http://www.freep.com/article/20090619/NEWS07/906190337/Continental+Airlines+pilot+dies+during+flight++plane+able+to+land+safely

No comments: