Thursday, September 03, 2009

Chadema wazindua mkutano kwa kishindo




CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) leo kimeanza mkutano wake mkuu utakaoendelea hadi kesho kumchagua Mwenyekiti wake wa taifa ambapo pia kimezindua programu ya kusajili wanachama kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu ijulikanayo kama ‘Electronic Membership’.(Cheki wanachama hapo juu pichani walivyocharuka).

Mbali na uzinduzi wa utaratibu huo ambao ni wa kwanza barani Afrika, chama hicho pia kimezindua vitabu viwili, “Programu ya Chadema ni Msingi” na “Programu ya Mafunzo ya Wanachama na Viongozi”.

Vitabu hivyo vinalenga kuwa na mwongozo mmoja kwa viongozi wote wa chama hicho nchini.

Akizungumza katika mkutano mkuu wa chama hicho uliofanyika kwenye ukumbi wa Shule ya Sekondari ya Mbezi Beach, mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema usajili wa wanachama kwa njia ya simu, una lengo la kukusanya wanachama milioni moja kabla ya kuisha kwa mwaka huu.

“Gharama ya kutuma ujumbe mfupi itakuwa ni Sh300 kwa ujumbe wa simu, fedha ambazo zitaweza kuwasaidia wabunge na madiwani wetu. Hatutaki kuwa na viongozi ambao wanatumia fedha zao kwa ajili ya kuwawezesha kwenye kampeni na shughuli mbalimbali za chama,” alisema Mbowe.
Alisema utaratibu wa kuwa na matawi ya wanachama umepitwa na wakati kwani matawi hayo siku hizi yamegeuzwa kuwa vijiwe vya uhalifu.

“Mashina ya wakereketwa siku hizi yamekuwa vijiwe vya wahalifu. CCM wanatakiwa watambue kwamba programu hii haiwezi kuundiwa zengwe na wakitufuata huku watakuwa na sababu zao. Lakini wao pia wajifunze kuachana na matawi kwani nchi nyingi kama Kenya na Marekani wameshaachana na mtindo wa matawi,” alisema Mbowe
Habari ya Mussa Mkama na Fidelis Butahe, Picha na Venance Nestory

No comments: