Wednesday, October 24, 2012

Mauzo ya Nyumba za Mindu

 

SHIRIKA LA NYUMBA LA TAIFA


 
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
UUZWAJI WA NYUMBA ZA MRADI WA UJENZI WA MINDU, DAR ES SALAAM


Kwa mara nyingine tena Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) leo 24 Oktoba, 2012  limezindua rasmi mauzo ya nyumba katika mradi wake mpya wa Mindu, jijini Dar es Salaam. Ujenzi wa mradi huu ulianza rasmi mwezi Novemba mwaka 2011,  na unatarajiwa kukamilika rasmi Aprili 2013 na mteja kuweza kukabidhiwa nyumba yake mwezi Mei  2013, ikiwa ni miezi 18 baada ya kuanza ujenzi.

Mradi unatarajiwa kugharimu kiasi cha zaidi ya Shilingi bilioni 11 mpaka utakapomalizika, fedha zinazogharamiwa na Shirika kutoka vyanzo mbalimbali vya mapato ikiwemo fedha za mikopo ya benki.

Mradi huu uliopo  mtaa wa Mindu eneo la Upanga, takribani mita 100 kutoka Hospitali Kuu ya Taifa Muhimbili, una sehemu ya nyumba 60 za kuuzwa zilizopo kwenye majengo pacha ya ghorofa 15, uko sehemu zenye huduma zote muhimu za kijamii  zikiwamo hospitali, shule, maduka, na masoko.

Pia Mradi unatarajiwa kuboresha maisha ya wanunuzi wa nyumba hizi kwani upo karibu kabisa na katikati ya jiji na kwamba mnunuzi anaweza kwenda kazini bila kutumia gharama yoyote ya usafiri wa gari.  Aidha, nyumba zipo ndani ya uzio kwa ajili ya usalama wa wakaazi wake  na kuna maegesho ya magari ya kutosha.

Nyumba 60 tu zinazouzwa ambapo kila nyumba ina vyumba vitatu vya kulala, vyo vinajitegemea. Kila nyumba ina ukubwa wa mita za mraba 141 (sq.m), sebule iliyoungana na eneo la kula chakula, choo cha umma, jiko kubwa la kisasa na eneo la kufulia na kuanikia nguo.

Sifa za ziada za mradi huu ni kuwa na eneo maalum la kukusanyia taka, sehemu iliyotengwa maalum kwa ajili ya kufanyia mazoezi (gym), bwawa la kuogelea (swimming pool) na eneo kubwa la ziada la maegesho ya magari.

Kila nyumba itauzwa kwa bei ya TZS  272,050,673.08 bila kodi ya ongezeko la thamani (VAT )  na  TZS  321,019,794.24 ikiwa na kodi ya ongezeko la thamani (VAT).
Tunawahamasisha na kuwakaribisha watanzania wote walio nchini na nje ya nchi kujitokeza ili kununua nyumba hizo. Wanaweza kufanya mawasiliano na Makao Makuu ya Shirika, Ofisi zetu za Mikoa au kupitia barua pepe na kukamilisha taratibu mapema kwa ajili ya kuweza kuingia kwenye mchakato ulio wazi wa manunuzi.
Katika kutekeleza miradi ya ujenzi wa nyumba, Shirika linajenga nyumba za gharama ya juu, kati na chini ili kuwahudumia watanzania wa kada zote. Katika azma hiyo, nyumba 10,000 zitakazojengwa kufikia 2015 zitahusu watu wa  kipato cha juu na nyumba 5,000 zitakazojengwa kufikia mwaka huo zitakuwa ni nyumba za watu wa kipato cha chini.

 Shirika limeanza kujenga nyumba za gharama ya kati na juu ili kupata faida itakayoliwezesha kuwajengea watu wa kipato cha chini nyumba za gharama nafuu. Hii inatokana na ukweli kuwa Shirika halipati ruzuku toka serikalini ya kujenga nyumba kwa ajili ya wananchi wa kipato cha chini. Mradi huu wa Mindu tunaouzindua hii leo, ni moja ya miradi ya ujenzi wa nyumba za watu wenye kipato cha juu..
Ukiwa mdau na mnunuzi mtarajiwa, ama una ndugu/rafiki anayetamani kununua nyumba katika mradi huu, tafadhali waweza kutumia akaunti nambari : …….. au wasiliana na Kitengo cha Mauzo simu namba 0754 444 333; barua pepe: sales@nhctz.com na pia tembelea tovuti ya Shirika www.nhctz.com  kwa maelezo zaidi.

IMETOLEWA NA:
KITENGO CHA MAWASILIANO NA HUDUMA KWA JAMII
SHIRIKA LA NYUMBA LA TAIFA







2 comments:

Unknown said...

Yaani nyumba Dar bei ghali kuliko Marekani? Whaaaaaaat????

mzee wa mshitu said...

Siyo elimu tu kaka bali hata Afya kwa maana ya matibabu, elimu ya aina yoyote ile, maana kindergaten siku hizi ni kama chuo kikuu, usafiri ukipanda ndege kutoka dar kwenda mwanza nighali kuliko hata toka new york pengine kwenda hata washington kwa maana ya internal flight. Namba yangu nimekurushia kaka yako kila nikipiga sikupati sijui kuna sehemu nakosea najaribu tena hiyo hapo 0784746157