Wednesday, November 11, 2009

Zaidi ya watu 20 wapoteza maisha kwa kuangukiwa na mlima

MVUA kubwa iliyonyesha usiku wa kuamkia jana wilayani Same, imeleta maafa makubwa baada ya watu 30 kuhofiwa kufa kufuatia kitongoji chao kuporomokewa na mlima ambao ulizifunika kabisa nyumba zao wakiwa usingizini.

Kazi ya ukoaji ambayo ilikuwa ikifanywa kwa kutumia vifaa duni yakiwemo majembe ilikuwa ikiendelea ambapo hadi kufikia jana saa 9:00 mchana, miili ya watu 16 ilikuwa imeopolewa kutoka katika vifusi vya mlima huo ulioporomoka.

Mkuu wa wilaya ya Same, Ibrahim Marwa alisema kuwa hadi kufikia saa 9:30 alasiri, idadi ya maiti waliokuwa wameopolewa ni 16 na kulikuwa na majeruhi nane waliookolewa katika jitihada zilizofanywa na wananchi waliofika mapema eneo la tukio.

“Kwa takwimu ambazo tumepata ni kwamba idadi ya waliokufa inaweza kufikia 25 hivi japo hatuna uhakika lakini wapo majeruhi tisa ambao wanahudumiwa hapa hapa na timu ya madaktari na wataalamu wa Afya kutoka Same,”alisema mkuu huyo wa wilaya.

Alifafanua kuwa chanzo cha maafa hayo ni mvua nyingi zilizonyesha mfululizo kwa siku tatu na kufanya mlima huo kushindwa kuhimili na kuporomokea nyumba saba za wananchi wa kitongoji hicho na kuzifunika kabisa wakati wamelala.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Mamba Miamba kulipotokea maafa hayo, Michael Chikira Mauya aliliambia Mwananchi kutoka eneo la tukio kuwa inakadiriwa nyumba hizo zilizofunikwa zinakadiriwa kuwa na familia za watu kati ya 20 na 28.

“Mpaka sasa hivi (saa 6:00 mchana jana) tumefanikiwa kutoa miili 12 na tunakadiria katika nyumba saba zilizofunikwa kunaweza kuwe na watu hadi 28 hivi…kwa kweli ni tukio ambalo ni baya sana hapa kijijini”alisema Diwani Mauya.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Kilimanjaro, Lucas Ng’hoboko, maofisa wengine wa polisi na askari wa vyeo vya chini na pia mkuu wa wilaya ya Same, Ibrahim Marwa walikuwa katika hekaheka za kuopoa miili ya waliokufa kutokana na janga hilo.

Tukio hilo limekuja wakati mvua ambayo imenyesha kwa siku tatu mfululizo katika kata za Maore, Ndungu, Kihurio, Bendera ikiwa imesababisha maafa makubwa na kusababisha vifo vya wanafunzi wawili ambao walisombwa na maji.

No comments: