Wednesday, November 18, 2009

Nnauye ahadharisha wauza 'unga' kufadhili vyama



MJUMBE wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Nape Nnauye, amesema vitendo watu wanaojihusisha na biashara ya madawa ya kulevya kufadhili vyama vya siasa katika uchaguzi mkuu, vinasababisha serikali inayoingia madarakani kutekeleza matakwa ya wafadhili hao.

Nape alisema hayo jana jijini Dar es Salaam, alipokuwa akizundua Chama Kuweka na Kukopa cha Upendo Group ambapo alisema serikali inayochaguliwa kwa njia hiyo itakuwa ya wauza madawa ambao maamuzi yao hayawezi kuleta maendeleo kwa wananchi.

“Hao wauza unga wanapopata nafasi ya kukifadhili chama cha siasa kisha chama hicho kikafanikiwa kuingia madarakani kwa nguvu za pesa zao, serikali ya chama hicho haitakuwa na uwezo wa kuwachukulia hatua watu hao na badala yake, itafanya maamuzi kwa muujibu wa wafadhili hao,”alisema Nnauye.

“Tukumbuke waswahili walisema “anayemlipa mpiga zumari ndiye anayechagua tuni ya muziki, wafadhili wa aina hiyo wakifanikiwa kukiweka chama madarakani kwa njia fedha zao, wanaweza kuichagulia serikali mambo ya kufanya kwa mgongo wa fedha zao,” alisema.

Kwa muda sasa, kumekuwa na hoja kuwa vyama vya siasa nchini, vinategemea kupata fedha za kampeni kutoka kwa wafadhili wao bila kujali nyanzo vya fedha hizo na athari zake kwa taifa.

Hata hivyo Nape ambaye alitoa Sh1.2milioni ili kukiwezesha upendo group kufungua saccos yao alisema vyama vya siasa visivyo kuwa makini na watu hao kuna siku vitajutia. Imeandikwa na Jackson Odoyo.

No comments: