Tuesday, November 10, 2009

Viongozi Daruso wafutiwa kesi

MAHAKAMA ya hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam jana wamewaachiwa huru viongozi watano wa serikali ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (Daruso), waliokuwa wanakabiliwa na kesi ya kufanya mkusanyiko usio halali.

Hakimu Mkazi, Victoria Nongwa aliwaachia huru wanafunzi hao kwa kile alichosema kuwa upande wa mashtaka kumeshindwa kupeleka shahidi hata mmoja wa kutoa ushahidi dhidi ya kesi hiyo.

Akiwaachia huru wanafunzi hao, hakimu Nongwa alisema kwa kuwa upande wa mashtaka umeshindwa kuleta shahidi hata mmoja kutoa ushahidi dhidi ya washtakiwa hawa, mahakama inawafutia shtaka watuhumiwa wote na kuwaachia huru.
Walioachiwa huru ni pamoja na rais wa Daruso, Antony Machibya, mbunge na katibu wa mtando wa wanafunzi wa Vyuo vikuu Tanzania, Owawa Steven Juma, mbunge wa Daruso, Sabinian Pricepius, Taitas Ndula na Apolo Issa ambao wote walikuwa wakitetewa na Wakili Furgens Massawe.

Awali washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo kwa tuhuma za kufanya mkusanyiko usio halali kinyume na kifungu cha sheria cha 71(1) na cha 75 cha Kanuni ya Adhabu kilichofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Watuhumiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kuwa Februari 9, mwaka huu saa 9:45 mchana kwa nia ya kutenda kosa walibeba mabango yaliyoandikwa ‘Laiti Nyerere angefufuka leo angelia machozi ya damu kweli, Kikwete umesahau umaskini wa watanzania wako, Hivi Pinda kweli wewe ni mtoto wa mkulima ?, wazazi wetu tuoneeni huruma tunateseka wanenu, vyuo vya umma vimeuzwa kwa matajili’ .

Maneno hayo yanadaiwa na upande wa mashtaka kuwa yanaleta uchochezi na uvunjifu wa amani.

Wakati wanafunzi hao wakisomewa maelezo ya awali yanayohusiana na kesi hiyo upande wa mashtaka ulijigamba kuwa utapeleka mashahidi sita ambao ni SSP Gervas Mapunda, SP Nganyisa, Ditectivu Gervas, PC Hamis, PC William na PC Nsajigwa.

Kesi hiyo namba 20 ya mwaka huu ilifunguliwa kwa mara ya kwanza Januari 21, mwaka huu katika mahakama ya hakimu mkazi Kisutu. Habari imendikwa na Tausi Ally wa gazeti la Mwananchi.

No comments: