Sunday, February 01, 2009

Mtoto aunguzwa moto na mama yake



KISA,ALIMWAGA NUSU KILO YA MCHELE

POLISI katika Kanda Maalum ya Dar es Salaam, wanamsaka mwanamke ambaye ni mkazi wa Tabata Dar West, kwa tuhuma za kumuunguza usoni kwa moto, mtoto wake wa miaka wa umri wa miaka saba.

Taarifa zilizolifikia gazeti hili jana na kudhibitishwa na askari mmoja wa Kituo cha Polisi cha Tabata, zilisema mwanamke huyo, alitoweka mara baada ya tukio hilo.

"Mama wa mtoto huyo alikimbilia mahali kusikojulakana, walimu katika shule anayosoma mtoto huyo ya Mtambani, wanamsaidia kufuata taratibu za kisheria ili mama yake, akamatwe na kufikishwa katika vyombo dola,"alisema askari huyo.

Askari huyo aliwashauri walimu hao, washirikiane na mjumbe wa aneo ambalo mwanamke huyo amekuwa akiishi, ili waweze kumkamata.

Akizungumzia tukio hilo, Mwalimu Wilbert, ambaye aliyewasilisha taarifa hizo polisi, alisema walipomhoji mtoto kuhusu tukio hilo, alidai mama yake alimuunguza baada ya kumwaga nusu kilo ya mchele, aliyokuwa amemtuma kwenda kununua dukani.

Alisema walipomwita mzazi wa mtoto huyo, hakutokea na badala yake, alikwenda dada yake, ambaye alidai mdogo wake alikuwa anacheza na kwa bahati mbaya, akamwagikiwa na maharage.

Alisema walimu walimweleza kuwa mtoto aliunguzwa moto na kitendo hicho kilifanywa na mama yake, dada huyo alikuwa mkali dhidi ya mtoto na kumtaka aseme mengine ambayo hakusema.

Kwa mujibu wa mwali huyo, ghafla baada ya muda msichana huyo alinyanyuka na kukimbia na hatua hiyo ilikuja baada walimu kumtaka waende naye polisi kutoa maelezo.

Mtoto huyo alisema tangu taarifa hizo zifikishwe polisi, amekuwa akipewa vitisho na dada yake ambaye pia ameamua kumnyima chakula na kumtaka aende kulala walimu wake.

Tukio hilo limekuja siku kadhaa baada ya tukio mwanamke mmoja wa Kimara, kufunga mtoto wake sehemu za siri kwa kutumia super glue, kama njia ya kumwadhibu.

Hata hivyo mwanamke huyo alikamatwa na kufunguliwa mashitaka. Habari hii imendikwa na Koku David.

No comments: