Tuesday, February 03, 2009

Katibu Mkuu UN kutembelea Tanzania

KATIBU Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban Ki-Moon atatembelea Tanzania baadaye mwezi huu, imethibitishwa mjini Addis Ababa, Ethiopia.

Ban Ki-Moon amethibtisha mwenyewe kuhusu ziara hiyo ya siku mbili, kuanzia Februari 25, mwaka huu.

Katibu Mkuu huyo alitangaza ziara hiyo wakati alipokutana na kuzungumza na Rais Jakaya Mrisho Kikwete, katika Kituo cha Mikutano cha UNCC-ECA mjini Addis Ababa.

Viongozi hao wawili wako mjini Addis Ababa, Ethiopia, kuhudhuria mkutano wa 12 wa kawaida wa viongozi wa nchi wanachama wa Umoja wa Afrika (AU).

Ban Ki-Moon alisema atazuru Tanzania baada ya kumaliza ziara yake nchini Afrika Kusini.

Hii itakuwa ziara ya kwanza kwa Katibu mkuu huyo wa UN, kutembelea Tanzania.

Katika mazungumzo hayo, Ki-Moon, alimsifia Naibu Katibu Mkuu wa UN, Dk Asha Rose Migiro wa Tanzania, kwa kuwa mwanamke mchapa kazi.

No comments: