Tuesday, November 22, 2016

SERIKALI YAJIPANGA KUKUZA UCHUMI WA WAKAZI WA BUSOKELO

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akifafanua jambo kwa wakazi wa kata ya Mpata wakati alipokagua miundombinu ya barabara katika kata hiyo. 
Wakazi wa mwakaleli wakimsikiliza Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani (hayupo pichani). 
Mbunge wa Busokelo Mhe. Atupele Mwakibete akiongea na wananchi wa jimbo lake wakati Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani alipotembelea kukagua miundombinu ya barabara jimboni humo. 



Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akifafanua jambo kwa wananchi wa Kata ya Mpata wilayani Busokelo mkoani Mbeya ambao wapo tayari kutoa maeneo yao ili kupisha ujenzi wa barabara inayounganisha kata hiyo na eneo la Mwakaleli. 
Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS) Mkoa wa Mbeya Eng. Paul Lyakurwa akisisitiza namna atakavyoshirikiana na wananachi wa kata ya Mpata katika ujenzi wa barabara itakayofungua uchumi wa kata hiyo ambayo ni maarufu kwa uzalishaji wa ndizi na viazi. 
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akijibu maswali ya wananchi wa Mwakaleli waliotaka kujua hatma ya fidia zao katika mradi wa ujenzi wa barabara ya Katumba-Mbambo hadi Tukuyu.
Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani akijibu maswali ya wananchi wa Mwakaleli waliotaka kujua hatma ya fidia zao katika mradi wa ujenzi wa barabara ya Katumba-Mbambo hadi Tukuyu.
……………………………………………………………….. 

Serikali imesema itaijenga kwa kiwango cha lami barabara ya Katumba-Mbambo hadi Tukuyu KM 79.4 ili kuiunganisha kwa lami wilaya mpya ya Busekelo na Wilaya nyingine za mkoa wa Mbeya na hivyo kukuza uchumi wa wilaya hiyo. 

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng.Edwin Ngonyani amesema hayo mara baada ya kukagua ujenzi wa barabara hiyo unaendelea katika sehemu ya Lupaso hadi Bujesi KM 10 na kumtaka mkandarasi anayejenga barabara hiyo kampuni ya Chongqing International Construction Corporation (CICO) kuongeza kasi ya ujenzi huo kwa kuzingatia makubaliano yaliyopo kwenye mkataba. 

“Nawaomba wananchi wa Busokelo msimcheleweshe mkandarasi kufanya kazi yake kwa kuepuka vitendo vinavyoweza kuchelewesha ujenzi wa barabara hii kwa kufungua kesi za kudai fidia kwani kwa kufanya hivyo kunachelewesha maaendeleo ya ujenzi wa barabara hii”. amesema Eng. Ngonyani. 

Eng. Ngonyani amewataka wananchi wa Wilaya ya Busokelo kushirikina na viongozi wao na kutoa ushirikiano unaostahili ili kasi ya ujenzi wa baraba za lami katika maeneo yao isikwamishwe na wananchi wachache. 

Akiwa wilayani Busekelo Naibu Waziri huyo amekagua barabara za Kata ya Mpata na Luteba ambazo zinasimamiwa na halmashauri na kuahaidi kushirikiana na Wizara nyingine ili kuongeza kasi ya ujenzi wa barabara katika wilaya hiyo inayozalisha mazao mengi chakula na biashara yanayosafirishwa katika miji mikubwa nchini. 

Naibu Waziri Ngonyani amezungumzia umuhimu wa kuziunganisha wilaya za Makete na Busokelo kwa lami ili kurahisisha usafirishaji wa mazao na kukuza utalii katika hifadhi ya kitulo. 

Amemuagiza Meneja wa wakala wa barabara (TANROADS) mkoa wa Mbeya Eng. Paul Lyakurwa kushirikiana na halmashauri ya Busokelo katika baadhi ya miradi ili kuongeza kasi ya kuboresha barabara na hivyo kuhuisha uchumi wa wakazi wa wilaya hiyo. 

Naye Mbunge wa Busokelo Mhe. Atupele Mwakibete amemuomba Naibu waziri Ngonyani kuangalia namna ya kuijenga barabara ya Kata ya Mpata ili kuwezesha magari mengi yanayosafirisha gesi kufika kwa urahisi katika eneo hilo na hivyo kurahisha usafirishaji wa gesi,kuongeza ajira kwa vijana na kuongeza pato la halmashauri hiyo. 

“Mhe. Waziri wananchi wa Mpata na Luteba wako tayari kutoa maeneo yao bila fidia ili barabara ijengwe katika eneo hilo ambalo ni muhimu kwa uzalishaji wa viazi na ndizi”. Amesistiza Mwakibete. 

Naibu waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonuani yupo katika ziara mikoani ya nyanda za juu kusini kukagua miradi ya ujenzi na kutoa maelekezo kwa taasisi zilizopo chini ya Wizara hiyo.

No comments: