Tuesday, November 15, 2016

DKT. MGWATU AAGIZA UKARABATI WA MASHINE ZA KUCHONGA VYUMA TEMESA MBEYA

Meneja wa Wakala wa Ufundi na Umeme TEMESA Mbeya Mhandisi Charles Irege (kushoto) akimuonyesha Mtendaji Mkuu wa TEMESA Dkt. Mussa Mgwatu (Kulia)mojawapo ya mashine ya uchongaji vyuma iliyo katika karakana ambayo inahitaji ukarabati. Picha na Theresia Mwami TEMESA Mbeya.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme – TEMESA Dkt. Mussa Mgwatu (kushoto) akitoa maagizo ya namna ya kuboresha huduma za ukodishaji mitambo kwa Meneja wa TEMESA Mbeya Mhandisi Charles Irege (kulia), alipotembelea kituoni hapo.


Na Theresaia Mwami TEMESA Mbeya

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi na Umeme TEMESA Dkt. Mussa Mgwatu amemuagiza Meneja wa TEMESA Mbeya Mhandisi Charles Irege kuhakikisha kuwa Mashine zote zilizo kwenye karakana ya kuchonga vyuma zinafanyiwa ukarabati ndani ya miezi miwili ili kuongeza uzalishaji.

Dkt. Mgwatu ameyasema hayo alipotembelea Karakana ya TEMESA iliyopo Jijini Mbeya na kukuta mashine nyingi za uchongaji vyuma ni mbovu na hazifanyi kazi.“Mnakosa fursa nyingi za kuongeza mapato kwa kushindwa kutengeneza vipuri mbali mbali vya wateja wakati huu ambapo Jiji la Mbeya linakuwa kwa kasi kiuchumi” Alisema Dkt. 

Dkt. Mgwatu ameongeza kuwa atafuatilia kwa ukaribu kuona kwamba mashine hizo za kuchonga vyuma zinafanyiwa ukarabati na kuanza kufanya kazi ipasavyo.

Katika hatua nyingine Dkt. Mgwatu amemtaka Mhandisi Irege kusimamia vyema kitengo cha ukodishaji mitambo kilichopo kituoni hapo, kutunza kumbukumbu sahihi za mapato na matumizi yatokanayo na ukodishaji mitambo na kuzuia mianya ya uvujishaji wa mapato ili kukuza pato la TEMESA Mbeya.

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Ufundi TEMESA yupo katika ziara ya nyanda za juu Kusini kutembelea na kukagua vituo vya TEMESA hicho ili kujionea changamoto na utendaji kazi.

No comments: